nEWS: Wizara ya Fedha na Mipango yaja na kanuni za usafirishaji, uingizaj na utoaji nje fedha taslimu...#share

WIZARA ya Fedha na Mipango imeandaa Kanuni za taarifa za Usafirishaji na uingizaji wa fedha taslimu kutoka na kwenda nje ya nchi  ambapo wasafirishaji wa fedha taslimu na wasafiri wote wanaotoka au kuingia nchini, watatakiwa kutoa taarifa za fedha taslimu wanazosafirisha ikiwa fedha hizo zinalingana au zinazidi kiasi cha dola za kimarekani elfu kumi (USD 10,000).


Akizungumza leo wakati wa ufunguzi wa warsha ya siku mbili ya maandalizi ya utekelezaji wa Kanuni hizo, Kamishna na Mtendaji Mkuu wa Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu (FIU) Onesmo Makombe amesema utekelezaji wa kanuni hizi, pamoja na mambo mengine utaiwezesha nchi kuwa na takwimu za usafirishaji fedha taslimu.

“Takwimu hizo zitakazosaidia pamoja na mambo mengine kubaini vitendo vya kihalifu, kupunguza utoroshaji wa mitaji na kuhakikisha kuwa tunapunguza kama siyo kumaliza kabisa usafirishaji wa fedha zitokanazo na uhalifu au/na fedha kwa ajili ya kufadhili ugaidi” amesema Makombe.

Aidha kanuni hizo zimeweka adhabu zitakazochukuliwa dhidi ya wale watakabainika kutaka kupita na fedha zinazolingana au zinazozidi kiwango kilichowekwa bila kutoa  taarifa au watakaotoa taarifa za uongo.  

Amezitaja adhabu hizo kuwa ni pamoja na kukamatwa kwa fedha taslimu walizonazo na kuchukuliwa hatua nyingine za kisheria kama vile kufunguliwa mashtaka. 

“Wahalifu pamoja na mambo mengine, wanapenda kusafiri na fedha taslimu kwani wanaogopa kutumia benki kutuma fedha kutokana na umakini unaoongezeka katika benki na udhaifu unaoweza kuwepo mipakani” Alisisitiza Bw. Makombe.

Kamishna huyo amewaasa washiriki wa warsha hiyo kutekeleza jukumu hilo  kwa uadilifu na uaminifu mkubwa ili kuziba mianya yote ambayo wahalifu wanaweza kuitumia kutimiza kusudi lao ovu na kuhatarisha usalama wa nchi.

Kutokana na umuhimu wa ushiriki wa wadau mbalimbali katika utekelezaji wa kanuni hizo warsha hiyo imejumuisha washiriki kutoka taasisi mbalimbali wengi wao wakiwa ni maafisa forodha.

Washiriki hao wametoka Wizara ya Fedha na Mipango, Wizara ya Fedha na Mipango-Zanzibar, Wizara ya Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki na kikanda, Mamlaka ya Mapato Tanzania na vikosi vya ulinzi na usalama

Wengine ni Bodi ya Mapato Zanzibar, Kikosi Maalum cha Kuzuia Magendo-Zanzibar, Shirika la Posta,  Benki kuu ya Tanzania, Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka-Zanzibar, Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka-Tanzania Bara Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania Bara na Zanzibar, Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania,  Idara ya uhamiaji na Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu.

Mwandishi Wetu

About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search