Patrobas Katambi aishushia tuhuma nzito Chadema....soma habari kamili na matukio360....#share

Na Abraham Ntambara, Dar es Salaam

ALIYEKUWA mwenyekiti wa Baraza la Vijana wa Chadema (Bavicha), Patrobas Katambi amedai lengo la kuundwa kwa Ukawa ni Chadema kuviua vyama vingine vya upinzani na  lengo hilo limefanikiwa.

Pia amesema wabunge 15 wa Chadema wanatarajia kukihama chama hicho na ameeleza sababu saba zilizofanya kujiondoa katika chama hicho
Aliyekuwa Mwenyekiti wa Baraza la Vijana Chadema (Bavicha) Patrobas Katambi akitoa sababu za kikihama chama mbele ya waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam, ametaja  sababu kuwa ni viongozi kushindwa kukijenga chama kuwa taasisi na  kinaendeshwa kibinafsi.

Nyingine ni ukosefu wa maamuzi shirikishi, ukiukwaji wa katiba na misingi ya kidemokrasia, ukosefu wa mawasiliano na umoja, ukosefu wa maadili ya kiuongozi, ufujaji na matumizi mabaya ya mali za chama na fedha na chama kukosa ajenda za kitaifa.

Katambi amesema ameamua kutoa ufafanuzi huo kutokana na upotoshwaji ambao umekuwa ukifanywa na viongozi na wanachama wa Chadema wakidai kwamba amenunuliwa.

Akizungumzia kuhusu wabunge hao 15, amesema  wapo njiani kukikimbia chama hicho kutokana na kutoridhishwa na namna kinavyoendeshwa na kwamba kwa sasa wanashindwa kufanya hivyo kutokana na kulinda maslahi au nafasi walizonazo ndani ya chama.

Kuhusu Ukawa;
Katambi amesema lengo la kuundwa kwa Ukawa lilikuwa ni Chadema kuviua vyama vingine vya upinzani ambapo ameeleza kuwa lengo hilo limefanikiwa.

“Kuundwa kwa Ukawa kulikuwa na makubaliano mawili ya ndani na nje, kwa nje wapo walioamini kuwa muungano huu utakuwa wa mapigano ya kitaifa, mfano CUF waliamini hivyo lakini kwa ndani Chadema lengo ilikuwa ni kuviua vyama vingine,” amesema.

Amesema hadi sasa lengo hilo limekamilika. Akitoa uthibitisho huo amesema ndiyo maana vyama vingine kama CUF, NCCR-Mageuzi na NLD viko dhofuli hali huku Chadema kikiwa na nguvu na kwamba kwa sasa Ukawa haupo tena.

Novemba, 2017 Katambi akiwa Mwenyekiti wa Baraza la vijana wa Chadema (Bavicha) mbele ya mkutano wa NEC alitangaza kujivua nyadhifa zote ndani ya chama cha Chadema na kujiunga na CCM kwa madai kutoridhishwa na mwenendo wa chama chake.





About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search