Vigogo uhujumu uchumi walia njaa Mahakamani...soma habari kamili na Matukio360

Na mwandishi wetu
Mkurugenzi wa Tathmini, Archard Alphonce Kalugendo (49) na Mthamini wa Madini ya Almas wa Serikali, Edward Joseph Rweyemamu (50) wameiomba Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu iwasaidie  kuzipata  kadi zao za Benki ambazo walinyang'anywa wakati walipokamatwa.


 Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu
Washtakiwa hao wametoa ombi hilo leo mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Respicius Mwijage wakati kesi hiyo ilipotajwa na wanaomba kurejeshewa kadi zao za Benki kwa sababu wanafamilia na mishahara yao inapitia huko, wasaidiwe kuzipata ili wasaidie familia zao.

Kufuatia ombi hilo, Hakimu Mwijage alimtaka Wakili wa Serikali, Simon Wankyo na wakili wa washtakiwa Nehemia Nkoko walifanyie kazi hilo ili familia za washtakiwa hao zisije kufa kwa njaa na kesi hiyo itakapotajwa wapeleke taarifa.

Awali, Wakili wa Serikali, Wankyo amedai  jalada la kesi hiyo ya uhujumu uchumi  linapangwa kwa ajili ya kupelekwa kwa Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) na kuna maeneo machache walikuwa wakiyafanyia kazi.

Hata hivyo amedai  tarehe ijayo wataeleza ni  hatua ipi waliyoifikia na akaomba ipangiwe tarehe nyingine kwa ajili ya kutajwa.
Wakili wa washtakiwa hao, Nehemiah Nkoko ameiambia Mahakama kuwa taarifa hiyo iliyotolewa na upande wa Mashtaka ni hatua nzuri na akaomba juhudi zifanyike katika upangaji wa hilo jalada.

Kesi hiyo imehahirishwa hadi  Novemba 9,2017. Washtakiwa hao wanakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi kwa  kusababisha hasara ya dola za Kimarekani 1,118,291.43 sawa na Tsh 2,486,397,982.54.

Kalugendo ambaye ni Mkazi wa Kinyerezi na Rweyemamu Mkazi wa Mwananyamala wote ni waajiriwa wa Wizara ya Nishati na  Madini.

Kati ya Agosti 25 na ,31, 2017 katika maeneo mbalimbali kati ya Dar es Salaam na Shinyanga, washtakiwa hao kwa pamoja na kwa vitendo vyao wakiwa wathamini walioajiliwa na Wizara ya Nishati na Madini walisababisha hasara ya kiasi hicho cha fedha.


Baada ya kusomewa shtaka hilo, washtakiwa hao hawakuruhusiwa kuongea chochote kwa sababu Mahakama ya Kisutu haina mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo hadi Mahakama Kuu. Washtakiwa wapo rumande.

About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search