Wachezaji Zanzibar Heroes wapewa viwanja, milioni tatu...soma habari kamili na matukio360..#share
Na Mwajuma Kombo, Unguja
RAIS wa Zanzibar, Dk Ali Mohammed Shein amewatunuku
wachezaji 33 wa timu ya taifa ya Zanzibar ‘Zanzibar Heroes’ kiwanja na
shilingi milioni tatu kila mmoja kufuatia kushika nafasi ya pili katika michuano ya Chalenji iliyofanyika nchini Kenya
Disemba 2017.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein, akiwa katika picha ya pamoja na wachezaji wa Timu ya Taifa ya Zanzibar Heroes wakati wa hafla ya chakula maalum alichowaandalia na kuwakabidhi zawadi.(Picha na Ikulu)
Hafla ya kukabidhi zawadi hiyo ilifanyika usiku wa
kuamkia jana katika viwanja vya Ukumbi wa Zamani wa Baraza la Wawakilishi
uliopo Kikwajuni mjini Unguja na kuambatana na taarab asilia iliyotumbuizwa na Kikundi cha Taifa cha
Taarab Zanzibar.
Viwanja hivyo walivyopewa wachezaji hao wametakiwa
kuvitumia wao wenyewe kwa ujenzi wa makazi na si kuviuza.
Akizungumza katika hafla
hiyo Dk. Shein alisema Zanzibar ni miongoni mwa nchi za Afrika Mashariki yenye
historia katika mpira wa miguu na hatua waliyofikia
wamedhihirisha hilo.
“Pamoja na kwamba nimetoa zawadi hizi lakini bado
zijaridhika sana, nilidhamiria niwapongeze kuliko hivi, dhamira yetu ilikuwa si
ya kushiriki ni ya kushinda na Zanzibar ilishinda”, alisema Dk. Shein.
Ameahidi kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
itajitahidi kuwekeza na kuiendeleza timu hiyo ili kuwa bora zaidi.
“Tutatafuta njia muhimu na walimu wetu tutawaongezea
nguvu ,
Zanzibar ina historia ya kuwa na walimu wazuri wa soka,”
alisema.
Pamoja na mambo mengine ameiagiza wizara ya Habari,
Utamaduni, Utalii na Michezo kuongeza kasi katika michezo
hasa kuandaa mipango kabambe ya mpira.
Aidha alikitaka chama cha soka Zanzibar (ZFA) kuacha kwenda mahakamani na kama mtu hawezi kuongoza
atoke ndani ya chama hicho kwani tabia ya kwenda mahakamani wanaiondolea
heshima Zanzibar katika soka.
Zanzibar ilishiriki michuano ya Chalenji inayoandaliwa
na CECAFA ambapo ilipata nafasi ya
pili baada ya kufungwa na Kenya ambao
ndio walikuwa wenyeji wa michuano hiyo kwa changamoto ya mikwaju ya penanti
3-2.



No comments:
Post a Comment