Maafisa jeshi la polisi wafundwa....soma habari kamili na matukio360....#share

Na
Abraham Ntambara, Dar es Salaam
JESHI la
Polisi nchini limewataka maofisa wa jeshi hilo zaidi 50 kutoka Tanzania Bara na
Zanzibar waliopata mafunzo ya ushauri nasihi katika dawati la jinsia kutumia
maarifa waliyopata kwa uadilifu na nidhamu ili kutatua changamoto zinazoikabili
jamii.
Pichani ni walioshiriki mafunzo ya siku tano ya ushauri nasihi katika dawati la jinsia jijini Dar es Salaam.
Kauli hiyo
imetolewa jana jini Dar es Salaam na Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Makao Makuu
Benedict Wakulyamba alipokuwa akifunga mafunzo hayo ya siku tano yaliyodhaminiwa
na Shirika la Utu wa Mtoto (CDF).
“Mafunzo
haya kama jeshi la polisi tumekuwa tukiyahitaji na lengo kuu la taaluma hii ni
kujiweka katika mazingira mazuri ya kuisaidia jamii, jambo la msingi ni
uadilifu na nidhamu ya hali ya juu,” amesema SACP Wakulyamba.
Amesema lengo
la kutumia maarifa hayo kwa uadilifu na nidhamu ni kutokana na kwamba wamepewa
dhamana ya kusikia na kujua siri na changamoto za watu wengine hivyo wanatakiwa
kuwasaidia wanajamii pasipo kutoa siri za matatizo yao nje.
“Itakuwa ni
jambo la kushangaza kama utaona na kusikiliza tatizo la mtu na kulitangaza
badala ya kusaidia na kulifanya kuwa siri baina yako na mwenye tatizo,”
amesema.
SACP
Wakulyamba ameeleza kuwa jamii imekuwa ikikabiliwa na changamoto mbali mbali
zikiwemo za kisaikolojia hivyo moja ya majukumu ya maofisa hao ni kupenyeza
elimu waliyopata ili kusaidia kuzauia matatizo ambayo yanaweza kuzuilika.
Kwa upende
wake Meneja Mipango wa CDF Dorothy Ernest, amesema kuwa tatizo la ukatili wa
kijinsia na watoto nchini bado ni kubwa na kwamba wamekuwa wakipambana nalo kwa
muda mrefu na kueleza kuwa mafunzo hayo yatasaidia kwa kiasi kikubwa
kukabiliana na changamoto hiyo.
“Mafunzo
haya yatasaidia kuboresha madawati ya jinsia na watoto nchini ili kuutokomeza
ukatilii huu wa kijinsia na tutaendelea kushirikiana na jeshi la polisi,”
amesema.
Ameongeza kuwa
katika mwaka huu wataendelea kuboresha madawati ya jinsia kwenye maeneo mbali
mbali nchini hususani katika kupata taarifa ambapo alisema kila mmoja
akiwajibika tatizo hili linaweza kutokomezwa.
Akizungumza kwa niaba ya wenzake Inspekata Amina Daffa kutoka Mkoa wa Kipolisi Ilala jijini Dar es Salaam, ameshukuru kwa mafunzo hayo na kwamba watayatumia vizuri katika kuhakikisha wanaisaidia jamii ili kuondokana na tatizo la ukatili wa kijinsia na changamoto mabli mbali zinazoikabili.
No comments:
Post a Comment