DK. Mwakyembe afichua siri kanuni mpya za maudhui...soma habari kamili na matukio360...#share

Na Mwandishi Wetu, Dodoma
SERIKALI imesema kanuni mpya za maudhui kwenye mitandao, runinga
na redio zimetungwa kwa lengo la kudhibiti usambazaji wa kauli chafu, matusi,
picha za utupu na zenye maudhui yasiyofaa kwa watoto.
Kanuni hizo zimetungwa ikiwa ni utekelezaji wa Sheria ya
Mawasiliano ya Kiektroniki na Posta ya Mwaka 2010.
Pia imesema itaendelea kuhamasisha utengenezaji na uzalishaji wa
maudhui ya ndani yanayozingatia maadili, mila na desturi za Mtanzania huku
ikikiri kuwapo kwa mmomonyoko wa maadili kunakoongezeka siku hadi siku, hivyo
imejipanga kukabiliana na changamoto hiyo.
Akiwasilisha bungeni mjini hapa jana hotuba ya makadirio ya
bajeti ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Waziri wa wizara hiyo,
Dk. Harrison Mwakyembe, alisema kanuni hizo zinamtaka kila mtumiaji wa mitandao
awe na namba ya siri ili 'wajanja' wasitumie kirahisi chombo chake cha
mawasiliano kutenda matendo yanayokwenda kinyume cha sheria.
Alisema kanuni hizo pia zinaweka muda maalumu kwa picha mgando
na nyongevu za filamu au muziki wenye maneno yasiyofaa kwa watoto kuonyeshwa
kwenye runinga.
"Tuliweka muda huo maalumu kuanzia saa 4:00 usiku hadi saa
11:30 asubuhi, lakini wadau wamekuwa wakali, wanadai picha na nyimbo hizo
zirushwe kuanzia saa 6:00 usiku wakati watoto wamelala na mwisho saa 11:00
asubuhi, kabla watoto hawajaamka," alisema Dk. Mwakyembe.
Aliongeza kuwa kanuni hizo zinataka madaraja yawekwe kwa kila
filamu, video, wimbo au albamu kutoka ndani au nje ya nchi ndipo kazi hizo
zitumike kwenye vyombo vya utangazaji.
"Msingi wa kanuni hizi ni kuhakikisha teknolojia
inatutumikia badala ya kututumikisha na kuvuruga mustakabali wa maadili ya
taifa letu. Ni kanuni zilizozingatia mazingira yetu halisi kama kila
Watanzania," alisema.
Dk. Mwakyembe alisema, mmomonyoko wa maadili ya Kitanzania
unaoongezeka siku hadi siku, ni miongoni mwa changamoto zinazoikabili wizara
yake.
Alisema wanaendelea kutoa elimu kupitia vyombo vya habari na
kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa kuzingatia maadili, mila na desturi za
Kitanzania.
Ili kutekeleza majukumu yake kwa mwaka ujao wa fedha, Dk.
Mwakyembe aliliomba Bunge kuidhinisha bajeti ya Sh. bilioni 33.3. Kati yake,
Sh. bilioni 12.2 ni mishahara, Sh. bilioni 9.3 kwa ajili ya matumizi mengine na
Sh. bilioni 8.7 za utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
No comments:
Post a Comment