Kitaifa: Wenye vyeti feki waachwa njia panda, Serikali yasema hatima yao ni baada ya mchakato wa uhakiki wao kukamilika...#share


WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora,  Angellah Kairuki amesema Serikali haijatoa tamko kuhusu hatma ya mafao ya watumishi wa umma waliokutwa na vyeti feki huku akibainisha tamko litatolewa baada mchakato wa uhakiki vyeti hivyo kukamilika.


Kauli hiyo ameitoa leo jijini Dar es Salaam wakati akizungumza na Watumishi wa Manispaa ya Kinondoni, amesema kumekuwepo na taarifa za upotoshaji kwenye mitandao ya kijamii zikieleza kwa namna tofauti tofauti jambo hilo, hali inayosababisha sintofahamu miongoni mwa wahusika na kusisitiza ufafanuzi utatolewa uhakiki utakapokamilika.

"Hakuna sehemu tuliyosema watalipwa au hawatalipwa mafao yao ifikapo mwisho wa uhakiki Serikali itatoa ufafanuzi," alisema Kairuki.

Waziri Kairuki amewataka watumishi wa manispaa nchini kuacha tabia ya kusambaza taarifa za Serikali kwani kufanya hivyo ni kwenda kinyume na Sheria ya Makosa ya Mtandao ya mwaka 2015.

Ameongeza kuwa changamoto zinazoikabili manispaa ya Kinondoni zitatafutiwa ufumbuzi zikiwemo za upungufu wa  walimu 50 wa shule ya msingi, watumishi 371 wa afya pamoja na watumishi wa ardhi na mipango.

Amewakumbisha maafisa utumishi wa manispaa hiyo kuwafanyia uhakiki watumishi kabla yakuwaingiza katika mfumo malipo ya mishahara na kwamba Serikali kwenye bajeti ya mwaka 2017/18  kuanzia mwezi huu hadi wa tisa itatoa vibali 52,476 vya ajira mpya.

Amewashauri watumishi hao kujikinga na Ukimwi kwa kubadili mienendo yao pamoja na kushiriki kufanya mazoezi ili kujiepusha na magonjwa yasiyoambukiza.

Kwa upande wake Afisa Utumishi Mkuu wa manispaa hiyo, Anna Mwakalyelye alisema hadi sasa mashauri ya nidhamu 134 yanashughulikiwa, 48 yameshashughulikiwa huku 80 yakiendelea kufanyiwa kazi.

Amesema manispaa tayari imeshatenga fedha za kujenga na kuzifanyia ukarabati Ofisi za kata zinazopatikana katka manispaa ya Kinondoni.
Amefafanua kuwa watumishi 372 walipandishwa vyeo na tisa kufanyiwa mabadiliko ya vyeo kulingana na vigezo walivyonavyo.

Pia amesema watumishi wanaendelea kupatiwa mafunzo ambayo lengo ni kuwasaidia kutekeleza majukumu yao ipasavyo.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Ali Hapi alimpongeza waziri Kairuki kwa utendaji kazi wake na kumuomba atizame kero zinazoikabili ikiwemo upungufu wa watumishi idara ardhi na mipango ambapo wanaofanya kazi wapo wanane wanaohudumia takribani watu milioni 1.3.


Na Hussein Ndubikile

About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search