Hotuba ya Maadhimisho ya Siku Ya Tembo Kitaifa Wilayani Namtumbo..

HOTUBA YA MWAKILISHI WA MKURUGENZI MKUU MAMLAKA YA USIMAMIZI WA WANYAMAPORI TANZANIA-TAWA.
KATIKA MAADHIMISHO YA SIKU YA TEMBO KITAIFA
MAMLAKA YA MJI MDOGO LUSEWA -WILAYA YA NAMTUMBO  TAREHE 22/09/2017
Bw.twaha twaibu mgeni rasmi kwa niaba ya katibu mkuu

Imesomwa na bwana Twaha Twaibu- Afisa Habari na Mawasiliano Mamlaka ya Wanyamapori Tanzania.
Mheshimiwa: Mkuu wa Wilaya ya Namtumbo,
Mheshimiwa: Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo,
Waheshimiwa: Madiwani,
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo
Katibu Tawala Wilaya ya Namtumbo
Wawakilishi wa Shirika la WWF Tanzania
Wenyeviti wa Serikali za Mtaa,
Watalaam wa maliasili,
Wawakilishi wa Jumuiya za Hifadhi (WMA),
Wawakilishi wa Taasisi mbalimbali,
Waandishi wa habari,
Wageni waalikwa
Mabibi na Mabwana:

Ndugu Wananchi;
Awali ya yote nachukua nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya njema na kuweza kukutana leo hii mahala hapa na hivyo kutuwezesha kupata fursa hii muhimu ya kuadhimisha siku ya Tembo Kitaifa  Wilayani Namtumbo.

Pili natoa shukurani zangu za dhati kwa Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo  na Shirika la WWF-Tanzania kwa kuandaa tukio hili. Pia natumia fursa hii kuwakaribisha watu wote waliotoka nje ya mji wetu wa Namtumbo kushiriki nasi katika maadhimisho haya muhimu kwa Tembo na maliasili kwa ujumla, karibuni sana.

Ndugu Wananchi;
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara yake ya Maliasili na Utalii ilitamka tarehe 22 Septemba, ya kila mwaka kuwa siku ya maadhimisho ya tembo kitaifa. Leo hii wana-Namtumbo  tunaungana na Watanzania wengine kuadhimisha siku hii  kitaifa.

Ndugu Wananchi;
Chanzo cha siku hii ya  maadhimisho ya tembo ilitokana na  mkutano wa 15 wa wanachama (COP15 ) juu ya  " Mkataba wa Biashara ya Kimataifa wa Viumbe Hai vilivyo hatarini kutoweka- “CITES” mkutano huu ulifanyika mwaka 2010 mjini Doha, Qatar. Katika mkutano huu nchi 37 barani Afrika zenye idadi kubwa ya Tembo zilipitisha mpango mkakati wa kuhifadhi tembo ulioitwa Mkakati Mkuu wa kuhifadhi tembo wa Afrika (African Elephant Action Plan – 2010).

Aidha, mwaka mmoja baadae (2011), Tanzania ilipitisha mpango wake wa kuhifadhi Tembo (Tanzania Elephant Management Plan 2010-2015). Tangu wakati huo, hapa nchini tunaadhimisha siku hii ya tembo kila mwaka.

Ndugu Wananchi;
Kitaifa, maadhimisho haya mwaka huu yanafanyika hapa wilayani Namtumbo Mkoa wa Ruvuma. Malengo ya kuyaleta  maadhimisho haya hapa ni kutokana na kuitaka jamii ya watu wa Namtumbo kushiriki katika kupamabana na ujangili na biashara haramu za vipusa na Meno ya Tembo. Pili Wilaya yetu ya Namtumbo, kijiografia inapakana na Pori letu kubwa la  Akiba la Selous. Na tatu ni kutokana na sehemu ya Wilaya ya Namtumbo kuwa moja ya mapitio makubwa ya tembo kutoka na kuingia katika Pori la Akiba la Selous nchini Tanzania na Pori la Taifa la Niassa Msumbiji.

Ndugu Wananchi;
Kauli mbiu inayoongoza maadhimisho haya kimataifa mwaka huu  ni “Be elephant ethical -BEE yaani Tuhifadhi Tembo kwa kuzingatia maadili yao”  Ujumbe huu unahamasisha jamii yote kwa ujumla, kuchukua hatua madhubuti na za makusudi ili kulinda maisha ya tembo na wanyamapori wengine kwani wanaunda sehemu muhimu ya mazingira yetu. Wizara ya Maliasili na Utalii, pamoja na wadau wengine hapa nchini na kote duniani, wanaendelea na jitihada za kulinda wanyamapori nchini. Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ameazimia kwamba “VITA DHIDI UJANGILI LAZIMA TUISHINDE”.

Ndugu Wananchi;
Kama nilivyosema hap awali madhumuni ya maadhimisho ya Siku ya Tembo kitaifa  ni kutoa fursa kwa jamii nchini kote kutambua na kuwa na uelewa wa pamoja wa masuala yanayohusu Tembo na wanyama pori wengine; Kuhamasisha watu wa jamii mbalimbali kushiriki kikamilifu kwenye maadhimisho haya na pia kuwa mstari wa mbele katika kuchukua hatua za kuhifadhi na kulinda wanyama wetu hasa tembo; Kutoa fursa kwa jamii kufahamu kwamba wao wana wajibu wa kuzuia ujangili na uwindaji haramu pamoja na uharibifu wa Mazingira; Kuhamasisha jamii kuelewa kuwa  usalama wa wanyamapori ni sambamba na usalama wetu sisi wenyewe, ukiachilia mbali kuwa jamii ya Watanzania kwa ujumla wao wananufaika kwa kipato cha fedha zakigeni  kupitia utalii.

Ndugu Wananchi;
Mwelekeo wa mauaji ya tembo nchini kwetu ni mbaya kutokana na uwindaji haramu wa tembo ndani na nje ya hifadhi zetu. Kwa mfano Pori la Akiba la Selous pekee limepoteza asilimia 90% ya tembo chini ya miaka 40 iliyopita, takribani tembo wapatao 110,000 wameuwa. Kwasasa tembo waliobakia wanakadiriwa kuwa 15,000. Inasemekana kuwa kama tukiacha ujangili huu uendelee kwa kasi hii tutakinyima kizazi kijacho fursa ya kufaidi vivutio na kufurahia urithi wa taifa.

Ndugu Wananchi;
Ili kutatua tatizo hili la ujangili nchini, tunahitaji ushirikiano wenu kwa kila hali na hususan katika kutoa taarifa juu ya uwepo wowote wa aina yeyote ya wageni na wenyeji wenye mwenendo wa kutia shaka katika kaya zetu na vijijini kwetu. Maana majangili hawatelemki toka hewani bali wanaishi miongoni mwetu.

Ndugu Wananchi;
Ninatoa wito kwa halmashauri zote nchini, taasisi zote za serikali, mashirika yasiyo ya kiserikali, na wananchi wote kwa ujumla kutumia fursa ya maadhimisho haya kushiriki katika kusimamia na kuhakikisha kuwa tunapinga kwa nguvu zote mauaji ya Tembo hapa wilayani Namtumbo na Tanzania kwa ujumla. Tutumie Kamati za Ulinzi  na Usalama na Maliasili na Mazingira za ngazi za vijiji, kata na wilaya kutambua na kusimamia mali asili ambazo ni urithi wa taifa letu.
Ndugu Wananchi;
Serikali inatambua majanga yaliyotokea mwaka huu 2017 yatokanayo na wanyama hawa tembo, kuna watu wamepoteza maisha, mali na mazao yao kuharibiwa na tembo. Kwa sasa serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii inakamilisha uhakiki wa mwisho kwani imebainika kuwa kuna mashamba hewa yaliyoingizwa kwenye orodha, uhakiki huo ukikamilika walioathirika watalipwa mara moja. Pia serikali inaandaa mpango kabambe dhidi ya majangili na kukabiliana na waanyama hawa ili wasiendelee kuharibu mazao na mali za wananchi pamoja na kulinda maisha ya wananchi dhidi ya tembo kwa njia za kisasa.

Ndugu Wananchi;
Napenda kuvipongeza vyombo vya habari kwa kazi nzuri ya uhamasishaji na ukuzaji weledi kwa wananchi kuhusu hali ya ujanglili nchini na hasa katika masuala ya kupingana na vitendo viovu. Naomba vyombo vya habari viendeleze juhudi hizi za kuelimisha umma kuhusiana na mapambano dhidi ya ujangili. Wanahabari wana nafasi kubwa na naamini mnaweza kutusaidia sana katika suala hili.

Ndugu Wananchi;
Napenda kutoa mwito kwa wadau wote wa uhifadhi nchini, halmashauri za wilaya, miji, majiji, taasisi za serikali na mashirika yasiyo ya kiserikali, kuongeza kasi ya kushirikiana katika kutokomeza tatizo la ujangili wa tembo nchini.

Ndugu Wananchi;
Suala la uhifadhi wa tembo ni mtambuka na linahitaji jitihada za pamoja kulitokomeza.  Hivyo basi ulinzi wa maliasili dhidi ya ujanglili ni jukumu letu sote linalotakiwa kufanyika kila siku. Nawaasa wananchi wote tuliohudhuria hapa tupinge na kuwafichua wale wote wanaojihusisha na vitendo vya hujuma kwa kuhusika na ujangili wa aina yeyote hapa wilayani Namtumbo na Tanzania kwa ujumla.
Hakika kwa pamoja, tunaweza kutokomeza ujangili wa aina yote nchini.

AHSANTENI KWA KUNISIKILIZA

M W I  S  H  O
===================

Wizara ya Maliasili na utalii imeyasifu juhudi za mashirika ya kimataifa ya uhifadhi.


Katibu mkuu wa wizara ya maliasili na utalii Mej. Jen. Gaudence S. Milanzi ameyasema kwenye siku ya Tembo Kitaifa iliyofanyika mji mdogo wa Lusewa wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma.


Katika hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na afisa wanyamapori Mkuu Bw. Twaha Twaibu kutoka mamlaka ya usimamizi wanyamapori-TAWA, Mej. Gen. Gaudence S. Milanzi amewasifu WWF kwa kuratibu maadhimisho hayo na juhudi zao katika kupambana na ujangili.

Watoto 3 waliyoshinda insha ya kuhifadhi tembo wakiwa na mgeni rasmi bw.twaha twaibu mwenye koti blue na viongozi wa wwf


Askari wanyamapori wa vijiji(VGS) kutoka vijiji vya Lusewa walihudhuria

Burdani kutoka kwa mrithi wa capt Komba bw.Neka anayeimbia TOT - Dsm

Mtoto toka sekondary ya Sasawala alikuwa wa kwanza kuandika insha ya kumuhifadhi tembo.pembeni ni Mkuu wa kikosi dhidi ujangili Songea Bw. Peter
Mkuu wa chuo cha likuyu Sekamaganga akisalimia wananchi Bi. Nyau
Bw. Peter anasoma hotuba ya kumwakilisha mkurugenzi mkuu wa TAWA.Bw. Peter ni mkuu wa kikosi dhidi ujangili Songea

About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search