Manji yamkuta mengine, Maya Manispaa ya Temeke adai amepoteza sifa kuwa Diwani...Kwa Kushindwa Kuhudhuria vikao...#share


MEYA wa Manispaa ya Temeke, Abdallah Chaurembo amesema mfanyabishara Yusuf Manji amepoteza sifa za kuwa Diwani wa Kata ya Mbagala Kuu kutokana na kutohudhuria vikao vya kamati vya halmashauri hiyo.


Amesema kwa kukosa vikao hivyo Manji ambaye kwa sasa yupo katika gereza la Keko akikabiliwa na kesi mbalimbali, amevunja  kanuni za Halmashauri pamoja na Sheria za Serikali za mitaa sura ya nane ya mwaka 1982.

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam, Meya Chaurembo alisema Manji amepoteza sifa kutokana na kutoshiriki vikao hivyo huku akisisitiza mfanyabiashara huyo alimuandikia barua Mkurugenzi wa manispaa hiyo Februari 20 mwaka huu ikitoa taarifa kutoweza kuhudhuduria vikao kwa sababu za kiafya bila kuwasilisha uthibitisho wa daktari.

''Vikao alivyokosa baada ya kuandika barua yake ni vile vya tarehe 3 na 4 vya mwezi Machi, 18-19/5/2017 na 24-25/8/2017  hivyo sheria za halmashauri za mwaka 2015 kifungu cha 72(c) ambacho kinatamka diwani pamoja na majukumu mengine aliyonayo lazima ahudhurie mikutano ya halmashauri na kamati ndogo ambayo yeye ni mjumbe bila kukaosa,'' amesema Chaurembo.

Amebainisha kuwa Mkurugenzi wa manispaa hiyo, Nassib Mmbagga alimwandikia barua mafanyabiashara huyo ikimtaka kuwasilisha taarifa za kidaktari kuthibitisha matatizo ya kiafya kama alivyoeleza kwenye barua yake lakini hakutekeleza huku akionekana kwenye vyombo vya habari akiendelea na shughuli zake.

Amesisitiza kuwa Manji aliandika barua Mei 22 mwaka huu kwa mkurugenzi ikieleza kutoweza kuhudhuria vikao hivyo kwa sababu za kiafya bila kuweka wazi uthibitisho wowote wa daktari na kwamba aliweka wazi nia yake ya kutaka kujiuzulu kama hali yake ya afya haitaimarika.

Ameongeza kuwa sheria za serikali hizo sura hiyo ya mwaka huo kifungu cha 25 (5) kinaeleza kuwa mjumbe wa Baraza la Madiwani ambaye hakuhudhuria vikao vtatu mfulilizo bila taarifa yoyote ya maandishi anajiondoa katika nafasi yake na kwamba kanuni za kudumu za manispaa za mwaka 2015 zinaeleza wazi kiti hicho kitakuwa wazi endapo mjumbe bila sababu ya kuridhisha au kibali cha maandishi cha mwenyekiti atakosa kuhudhuria mikutano mitatu nafasi yake inatakiwa kuwa wazi (kifungu cha 73 (1) (m).

Amefafanua kuwa Manji hakuhudhuria vikao vya mikutano ya halmashauri iliyofuatana bila kutoa taarifa ikiwemo ya Februari 3 mwaka huu, Machi 24, 2016, Juni Mosi mwaka jana,  Aggosti 25, 2016, Novemba 24,2016 na Februari 14 na 15 mwaka huu.

Aidha, amesema vikao vya  kamati ambayo yeye alikuwa mjumbe hakuhudhuria vya tarehe 18/3/2016, 17/8/2016,  8/11/2016 na 2/2/2017 huku akibainisha hata mikutano aliyotoa taarifa  alishindwa kuthiubitisha taarifa za ugonjwa.

Pia amesema tayari ameshamwandikia barua Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, George Simbachawene kumjulisha uvunjivu wa kanuni za kiutendaji uliofanywa na Manji hivyo waziri mwenye mamlaka ya kutangaza nafasi hiyo iko wazi.

Na Hussein Ndubikile


About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search