Wananchi, askari watunishiana misuli...Soma habari kamili na Matukio360


Na Salha Mohamed

NI kama filamu inaanza. Askari wakiwa na silaha za moto wakiwa barabarani huku wananchi wakiwa wanapiga kelele na kulalama wakidai wanataka haki zao.
Askari wa Jesho la Polisi na Wakazi wa Ukonga Mombasa jijini Dar es Salaam wakisubiri kumsikiliza Mkuu wa Wilaya Ilala Sophia Mjema.

Ndivyo imekuwa leo kwa wakazi wa Ukonga Mombasa eneo la Mazizini jijini Dar es Salaam, baada ya wananchi kufunga barabara kwa kile kinachodaiwa askari wa kikosi cha kutuliza ghasia (FFU), Ukonga kupiga na kujeruhi raia.

Oktoba 22 mwaka huu, eneo la Ukonga Mombasa, majira ya saa mbili usiku askari hao walianza kupiga kila raia aliyepo eneo hilo bila kujali umri, jinsia wala hali ya mwananchi.
Kupigwa kwa wananchi hao imedaiwa ni kulipa kisasi kwa kuuawa kwa askari mwenzao, PC Charles Yanga. 

Kifo cha askari huyo kilitokea Oktoba 21, mwaka huu ambapo mwili wake ulikutwa ukiwa kiwa na majeraha kwenye paji la uso na sikio moja likiwa limekatwa kabisa ukiwekwa pembeni mwa uzio wa kambi yao ukiwa ameanguka chini huku pikipiki yake aliyokuwa akiendesha ikiwasha taa za tahadhari (hazards light).

Kutokana na tukio hilo, askari hao waliingia eneo hilo nakuanza kumpiga kila raia wanayemuona mbele yao kwa rungu, mkanda na hata mateke na kuwasababishia majeraha makubwa na hata kuwavunja viungo (mguu).

Jambo hilo liliwafanya wananchi hao kukimbia hovyo na kufunga biashara zao mapema kutokana na hofu waliyokuwa nayo kwa kile kipigo wanachokiona au kukipata kwa askari hao.

Kipigo hicho hakikuwafurahisha wananchi jambo lililowasababisha kufunga barabara ya Mazizini hadi Moshi Bar kwa saa kadhaa huku wakidai amani kwani wameharibiwa mali zao huku wengine wakidai wameharibiwa kisaikolojia.

Baada ya kufungwa kwa barabara hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Ilala ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Usalama wilayani hapo, Sophia Mjema alifika eneo hilo na kuwasihi askari hao(FFU) kuondoka eneo hilo.

Baada ya askari hao kuondoka ndipo wananchi walipoanza kupaza sauti zao kwa kudai wameumizwa na pindi wanapokwenda polisi kuomba PF3 ili wakapate  matibabu hukataliwa.

Mjema aingilia kati Kutokana na vurugu hizo na shughuli za kibiashara kusimama eneo hilo, Mjema amewataka wananchi hao kuwataka askari waliohusika katika vurugu hizo ambapo watachukuliwa hatua kama kuhamishwa kikosi.

Wananchi hao walisema wanawafahamu askari waliokuwa wakiwapiga huku wakipaza sauti zao kwa kulitaja jina la askari mmoja aliyefahamika kwa JJ ambapo alichukuliwa kijana aliyejulikana kwa kwa jina la Jamal Yahaya kuwataja askari hao.
Wakazi wa Ukonga Mombasa wakimsikiliza Mkuu wa Wilaya ya Ilala (pichani hayupo)

Mjema amesema hakubaliani na kitendo cha askari hao kuwapiga raia kwami haijajulikana sababu ya kifo cha askari huyo.

"Jambo hili halikubaliki kama kuna tatizo lolote ambalo askari wanaliona kuna ngazi na taratibu za kisheria, wao kujichukulia sheria mkononi haikubaliki. Lazima hao askari waliofanya hivyo wachukuliwe hatua za kinidhamu na kisheria,"amesema.

Amesema wananchi walioharibiwa mali zao, walioumia wajiorodheshe ili waweze kuoata matibabu na mali zao."Wananchi watulie hili jambo si kubwa sana hadi wakoseamani lipo ndani ya uwezo wa serikali ya Wilaya wananchi watulie,"amesema.

Awali Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Kata ya Mazizini, Richard  Muhuza amesema aliwaona askari na kuwasihi kuacha kuwapiga wananchi lakini alishindwa kutokana na askari hao kuwa wengi.

"Askari walikuwa wamevaa soksi nyeusi, sare za jeshi, bukta, pensi wapo zaidi ya 50 walikuwa wanaingia hadi ukumbini kwenye sherehe wakisema tunawapiga wote hakuna cha sherehe kwanini askari mwenzao ameuawa.

"Walikuwa wanampiga kila mtu anayeshuka kwenye daladala, upo nyumbani umeacha mlango wazi wanakupiga na kuchukua fedha, sisi tulishindwa kwasababu walikuwa wengi wanamarungu bakora hawajui huyo mtoto wao wanapiga tu,"amesema.

Polisi walaani

Jeshi la Polisi Kanda hiyo, limelaani vikali vitendo hivyo ambavyo havina maadili ya kazi za Polisi huku likifungua jalada na uchunguzi kunaendelea ili kuwabaini watuhumiwa wa tukio hilo.

Kamanda wa Polisi wa Kanda hiyo,SACP Lazaro Mambosasa amesema “Tunaomba wananchi watoe ushirikiano kutoa taarifa za wahusika ili kuwachukulia hatua watu au askari waliohusika na matukio hayo ya kuwapiga wananchi kitendo ambacho ni kinyume na sheria za nchi,"amesema.

Amesema katika ufuatiliaji Polisi wamebaini askari huyo kauwawa na watu wasiojulikana  kisha kutelekezwa katika maeneo hayo ya kambi ya Polisi.

"Polisi kupitia kikosi kazi chake kinaendelea na msako mkali wa ufuatiliaji wa tukio hili la kinyama ili kuwabaini watuhumiwa waliohusika kutekeleza mauaji hayo na kufikishwa mahakamani ili kujibu mashtaka yanayowakabili,"amesema.

Wakati huo huo, Jeshi hilo limepokea malalamiko ya watu wanaosemekana ni askari kufanya msako na kuwapiga wananchi wanaoishi maeneo ya jirani na kambi ya Polisi kikosi cha kutuliza ghasia (FFU) ambao hawana hatia yeyote.



About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search