Waziri Ummy apokea vifaa vya saratani...soma habari na Matukio360..#share

Na Abraham Ntambara

TANZANIA inakabiliwa na changamoto ya kuwa na ongezeko la idadi kubwa ya wagonjwa na vifo vinavyotokana na saratani.

WAZIRI na Naibu Waziri wa  Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu na Dk. Faustine Ndugulile (wapo katikati) wakikabidhi vifaa tiba walivyopokea kwa Bohari ya Dawa (MSD) kwa ajili ya kusambazwa katika vituo vya afya.
 ...

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam wakati akipokea vifaa vya uchunguzi na matibabu ya awali ya saratani ya mlango wa kizazi, waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu amesema takwimu zinaonesha kila mwaka  takribani wagonjwa wapya 50,000  wanagundulika kuwa na saratani.


Vifaa  hivyo ni mashine 100  za tiba mgando  (cryotherapy) na mashine  tisa za upasuaji mdogo (LEEP) ambazo zitatumika kwa ajili ya matibabu ya awali ya saratani kwa wanawake watakaofanyiwa uchunguzi na kukutwa na mabadiliko ya awali ya saratani hiyo.

“Idadi hii inakadiriwa itaongezeka kwa asilimia 50 ifikapo 2020,” amesema Ummy.

Tarifa kutoka Taasisi ya Saratani ya Ocean Road kwa kipindi cha mwaka 2006 hadi 2015 zinaonyesha kwamba aina za Saratani zinazoongoza nchini ni  Saratani ya mlango wa kizazi asilimia 34, Saratani ya Ngozi (kaporsis Sarcoma) asilimia 13 na Saratani ya matiti asilimia 12.

Nyingine ni Saratani ya mfumo wa njia ya chakula asilimia 10, Saratani ya Kichwa na shingo asilimia 7, Saratani ya Matezi asilimia 6, Saratani ya Damu asilimia 4, Saratani ya Kibofu cha mkojo asilimia 3, Saratani ya ngozi asilimia 3, Saratani ya Macho asilimia 2, na saratani ya tezi dume asilimia 2. 

Amesema kutokana na takwimu hizo asilimia 80 ya wanawake wanaougua saratani hii wanafika katika vituo vya kutolea huduma za afya kwa ajili ya tiba wakiwa katika hatua za mwisho za ugonjwa, ambapo hufanya  matibabu kutokuwa na matokeo mazuri.

Ameongeza kwamba Serikali imekuwa ikitumia fedha nyingi kutibu wagonjwa  hao ambapo ameeleza kuwa Saratani ya Mlango wa kizazi inatibika endapo itagundulika mapema sambamba na kusaidia kupunguza gharama za matibabu ambazo Serikali, familia na mgonjwa wamekuwa wakikabiliana nazo.

Waziri Ummy amesema Kwa kushirikiana na wadau mbalimbali, Wizara imeshaanzisha vituo 459 (vituo 343 vya serikali na 116 vya mashirika na watu binafsi) vinavyotoa huduma ya uchunguzi na matibabu ya mabadiliko ya awali ya Saratani ya Mlango wa Kizazi.

Akizungumzia kuhusu vifaa alizopokea, amesema huo ni mkakati wa serikali Katika kuhakikisha  inaongeza upatikanaji wa huduma za uchunguzi na matibabu ya awali ya Saratani ya Mlango wa Kizazi.

Amewatoa hofu watanzania kuhusu gharama za matibabu kwa kusema kuwa huduma hizo zinapatikana katika Hospitali zote za Rufaa za Kanda na Mikoa, Hospitali zote za Wilaya, na baadhi ya Vituo vya Afya na Zahanati bure na kuwataka waganga wakuu wa Mikoa na Wilaya kuhakikisha wanatoa huduma hizo bila vikwazo.


About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search