Aliyepandikizwa figo Muhimbili aruhusiwa...soma habari kamili na matukio360..#share

Na Mwandishi Wetu

PRISCA Mwingira aliyefanyiwa upasuaji wa kihistoria wa kupandikizwa figo katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) ameruhusiwa kutoka hospitalini akiwa na afya njema.

Prisca Mwingira akimshukuru kaka yake, Bathelomayo Mwingira kwa kumpatia figo kutokana na tatizo hilo kumsumbua katika kipindi cha mwaka mmoja.

Alifanyiwa upasuaji huo mkubwa na wa kwanza kufanyika nchini ambapo alipandikizwa figo  Novemba 21, 2017 chini ya timu ya wataalam wa MNH kwa kushirikiana na watalaam wa Hospitali ya BLK ya nchini India.

Akizungumza na waandishi wa habari  leo baada ya kuruhusiwa kutoka Prisca amewashukuru watalaam wote walioshiriki katika kumuhudumia.

Pia ametumia fursa huyo kumuomba Rais John Magufulu kuendelea kuisaidia MNH ili kuhakikisha huduma za kibingwa  zinaendelea kutolewa katika hospitali hiyo.

“Kipekee namshukuru mwenyezi Mungu, madaktari, wauguzi, uongozi wa MNH pamoja na serikali kwa kufanisha matibabu yangu, nilisumbuliwa na ugonjwa wa figo takribani mwaka mzima na kuingia katika matibabu ya kuchuja damu, lakini hatimaye leo kaka yangu amejitolea figo yake moja na nimewekewa mimi kwa kweli namshukuru sana,”.

“Napenda kuwashauri wagonjwa wenye matatizo ya figo na wanaoendelea na huduma ya kuchuja damu wasikake tamaa kwani sasa matibabu yamepatikana na mimi ni shuhuda katika hili,’’ amesema.

Kwa upande wake, Bathelomayo Mwingira ambaye amemtolea figo dada yake,  amefurahi kwa kusaidia kufanikisha matibabu ya dada yake na kumuomba Mungu aendelee kuimarisha afya ya dada  yake.

Baba mdogo wa Prisca , Ainhard Mwingira ameishukuru serikali ya awamu ya tano kwa kufanikisha huduma za kibingwa  kutolewa Muhimbili.

Daktari Bingwa wa Magonjwa ya figo, Dk. Jackline Shoo wa Muhimbili amesema upasuaji wa kupandikiza figo ulitumia takribani saa nne na zoezi hilo limekamilika vizuri na mgonjwa anarejea nyumbani  huku afya yake ikiwa salama.

“Mgonjwa anaondoka hospitalini akiwa mzima salama kabisa,anaenda kujumuika na familia yake ataishi kama binadamu wengine ingawa kuna masharti atatakiwa kuyafuata  kama alivyoshauriwa na wataalam,” amesema Dk. Shoo.

Mkuu wa kitengo cha mawasiliano na huduma kwa wateja, Aminiel Aligaesha amesema upasuaji huo umegharimu  milioni 21 na endapo mgonjwa angepelekwa nchini India matibabu yake yangegharimu milioni 80 hadi milioni 100.

“Kwa niaba ya uongozi wa MNH nawapongeza watalaam wote walioshiriki katika upasuaji huu mkubwa na wa kihistoria na pia naishukuru serikali kwa kufanikisha zoezi hili,’’ amesema.


About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search