Kanisa la Kakobe linahifadhi fedha kwenye ndoo, jaba amuomba radhi Magufuli....soma habari kamili na matukio360..#share


Na Salha Mohamed, Dar es Salaam
MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) imesema kanisa la  Full Gospel Bible Fellowship,linaloongozwa na Zacharia Kakobe linatunza kiasi kikubwa cha fedha kwenye ndoo na majaba kinyume na taratibu za utunzaji wa fedha.

Pia imesema Kakobe aliandika barua kwa rais John Magufuli kuomba radhi kufuatia kauli yake ya kebehi  na matamshi ya dharau kwamba anafedha nyingi kuliko serikali.

Kamishna mkuu wa TRA, Charles Kichere akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam


Kamishna mkuu wa TRA, Charles Kichere amesema hayo leo jijini Dar es Salaam na kwamba askofu Kakobe hana fedha wala akaunti nchini ila ni mmoja wa wasimamizi wakuu wa akaunti za kanisa (Signatories) zilizopo kwenye benki ya NBC zenye kiasi cha sh bilioni 8.

Amesema kanisa  hilo linaweka na kutoa  fedha nyingi kutoka benki bila kushirikisha vyombo vya ulinzi na usalama kwa ajili ya usalama wa fedha na wahusika.

Kichere amesema kanisa hilo halitengenezi hesabu za mapato na matumizi ya fedha  kinyume  na katiba ya kanisa  na sheria za usimamizi wa fedha na kusababisha matumizi mabaya ya fedha za waumini kama safari za nje zinazoaminiwa na kanisa huku wanaosafiri ni Kakobe na familia yake.

"Vile vile fedha za kanisa zinatumika  kujenga nyumba ya mke wa askofu kwa jina lake wala si jina la kanisa jambo ambalo ni kinyume na taratibu za kanisa," amesema Kichere na kuongeza

"Wakati uchunguzi  ukiendendelea Januari 24,2018 Askofu Kakobe aliandika barua  kwa rais John Magufuli kuomba radhi kutokana na kauli yake ya kebehi pamoja na matamshi ya dharau kwamba anafedha nyingi kuliko serikali.’’

Kamishna huyo amesema uchunguzi umebaini kiasi cha sh bilioni 8  za kanisa hilo  zimetokana na sadaka, zaka na changizo ambazo zinatolewa na waumini wa kanisa na  kwa mujibu wa sheria hazitozwi kodi.

Amesema kanisa lilikwepa kulipa kodi ya sh milioni 20  zilizotokana na uwekezaji katika makampuni ya kukuza mitaji.

Ameongeza kuwa, Kampuni inayomilikiwa na watoto wa Askofu Kakobe ilikwepa kulipa kodi sh milioni 37.

"Kutokana na uchunguzi fedha zote walizokwepa kodi sh milioni 58 pamoja na faini zimelipwa,"amesema. 

Kichere ametoa wito kwa taasisi za dini zinazojihusisha na shughuli za kiuchumi kulipa kodi stahiki kwa wakati kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu za kodi.

"Mamlaka ya mapato Tanzania inazitaka taasisi zote za kidini kufuata katiba zao ikiwa ni pamoja na kutengeneza hesabu za mapato na matumizi, "amesema Kichere.

About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search