Kesi Madabida mabishano ya kisheria yatawala…soma habari kamili na matukio360...#share


Na Mwandishi Wetu

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu kesho inatarajia kutoa uamuzi katika kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili aliyekuwa mwenyekiti wa CCM mkoa wa Dar es Salaam, Ramadhani Madabida na wenzake watano  kama ina mamlaka ya kuisikiliza ama la.


Aliyekuwa mwenyekiti wa CCM mkoa wa Dar es Salaam, Ramadhani Madabida (kushoto).

Uamuzi huo unatarajiwa kutolewa na hakimu mkazi mwandamizi, Victoria Nongwa.

Ni baada ya kusikilizwa hoja zilizowasilishwa na upande wa Mawakili wa serikali, Pius Hilla na Shedrack Kimaro na Mawakili wa utetezi, Denis Msafiri,Makaki Masatu na Nehemia Nkoko.

Wakili wa Serikali  Kimaro akiwasilisha hoja alidai kuwa  hoja ya Mawakili wa utetezi kuwa mahakama ya Kisutu inamamlaka ya kuisikiliza kesi hiyo kwa sababu ipo chini ya bilioni 1 siyo sahihi.

Alidai kuwa ni dhahili kuwa makosa hayo ni ya uhujumu uchumi na mamlaka yenye mamlaka ya Kuisikiliza ni Mahakama Kuu Kitengo cha Rushwa na Uhujumu Uchumi maarufu mahakama ya Mafisadi.

Hivyo mahakama za chini kama Mahakama ya Kisutu haina mamlaka ya kuisikiliza kesi hiyo labda kuwepo na kibali cha kulipa mamlaka ya kuisikiliza kutoka kwa Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP).

Hivyo aliomba mahakama kutupilia mbali hoja za upande wa utetezi.

Wakili wa utetezi, Msafiri alidai kuwa ameusikia upande wa mashtaka, Ila ni rai yao kuwa marekebisho ya sheria ya uhujumu uchumi ya 2016 yanaipa moja kwa moja mahakama ya Kisutu kuisikiliza kesi hiyo.

Alidai kuwa kosa lolote lililopo chini ya Sh 1 bilioni haliwezi kusikilizwa na Mahakama Kuu Kitengo cha Rushwa na Uhujumu Uchumi ni Mahakama za chini ikiwamo Mahakama ya Kisutu.

Alisisitiza kuwa mahakama ya Kisutu inamamlaka kamili ya kuisikiliza kesi hiyo kwa vile shtaka halizidi Sh 1 bilioni na kwamba mahakama hiyo ndiyo yenye mamlaka ya kuisikiliza kesi hiyo na siyo Mahakama Kuu.

Pia alidai kuwa kibali cha DPP cha kuipa mamlaka mahakama kusikiliza kesi kinapaswa kipelekwe mahakamani pamoja na hati ya mashtaka.

Kesi hiyo imeahirishwa hadi Leo ambapo mahakama itatoa uamuzi na washtakiwa waliamuliwa wapelekwe polisi.

Hata hivyo, Wakili wa Serikali,Pius Hilla aliomba wapelekwe magereza kwa sababu washtakiwa hao  kuendelea kuwa mikononi mwa polisi kuna suala la gharama na polisi hawana fungu.

Baada ya kutolewa kwa ombi hilo, Wakili Nkoko aliomba mahakama kusimamia amri yake kama ilivyoitoa. 

Wakili Masatu  naye aliiomba mahakama iendelee na oda yake ilivyoitoa jana.

Hakimu Nongwa alisema suala la gharama hawawezi kulikwepa pale Haki inapotafutwa na kuamuru washtakiwa wapelekwe polisi hadi Leo atakapotoa uamuzi kama mahakama hiyo ina mamlaka ama la.

Madabida na wenzake wanakabiliwa na mashtaka sita  ya uhujumu uchumi ikiwamo kusambaza dawa bandia za kufubaza virusi vya Ukimwi ' ARV’s ' na kusababisha hasara ya Sh 148 milioni.


About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search