Scorpion jela miaka saba kulipa fidia milioni 30...soma habari kamili na matukio360....#share

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

MAHAKAMA ya Wilaya ya Ilala imemuhukumu Mwalimu wa sanaa ya kujihami, 'Martial arts' Salum Njwete maarufu kama  Scorpion,  kutumikia kifungo cha miaka saba jela  na kulipa fidia ya Sh milioni 30 baada ya kupatikana na hatia ya kujeruhi kwa kumtoboa macho, Said Mrisho.

Hata hivyo, mahakama hiyo ilimuachia huru kwa kosa la unyang'anyi wa kutumia silaha  baada ya upande wa mashitaka kushindwa kuthibitisha mashitaka hayo. 

Mwalimu wa sanaa ya kujihami, 'Martial arts' Salum Njwete maarufu kama Scorpion akitolewa mahakamani leo mara baada ya kukutwa na hatia katika kesi ya kujeruhi ikiwemo kumtoboa macho kinyozi Said Mrisho lkwenye mahakama ya wilaya ya Ilala jijini Dar es Salaam.

Akisoma hukumu hiyo leo, Hakimu Mkazi, Flora Haule amesema upande wa mashtaka ulileta mashahidi kumi huku mshtakiwa akijitetea  mwenyewe.

Amesema mshtakiwa ametiwa hatiani kwa kifungu namba 225 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu sura ya 16 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

Hakimu Haule alisema mahakama imejiridhisha kuwa mlalamikaji Said Mrisho  alishambuliwa kutokana na majeraha mbalimbali kwenye mwili wake ambapo madaktari walithibitisha.

"Mahakama imeridhika na ushahidi uliotolewa kwamba mshitakiwa ndiye aliyemjeruhi mlalamikaji kwani ni kinyume na sheria kujeruhi au kumuadhibu mtu hata kama ana makosa. Ushahidi umeonesha kuwa Scorpion alikuwa anajishughulisha na ulinzi ambapo uhalifu eneo la Buguruni umepungua kwa kazi yake," alisema Hakimu Haule.

Alifafanua kuwa dhamira ya mshitakiwa ilikuwa ni kupambana na mtu aliyemdhania kuwa ni mhalifu na sio nia yake kuiba, hata hivyo hakuna shahidi aliyeeleza kama mshitakiwa aliiba.

Kabla ya kutolewa adhabu, Wakili wa Serikali, Frank Tawale aliiomba mahakama kutoa adhabu inayostahiki kwa mshitakiwa kwa kuzingatia ulemavu aliosababishiwa mlalamikaji.

Tawale alidai kuwa Taifa limepoteza nguvu kazi kwa mlalamikaji kupata majanga hayo na kwamba  familia inamtegemea kwani hawezi kuwajibika na ndoto zake zimefifia.

Akitoa utetezi, Wakili wa mshitakiwa hugo, Hussein Hitu aliomba  mahakama impunguzie adhabu mshitakiwa kwa kuwa ni kosa lake la kwanza na ni mtu mwema kwa kuwa hata ushahidi umeeleza kuwa uhalifu eneo la buguruni ulipungua.

Hitu alidai mshitakiwa anafamilia inayomtegemea hivyo iangalie adhabu itakayotoa ili mshitakiwa  aendelee na shughuli nyingine. 

Hata hivyo, Hakimu Haule alisema mshitakiwa atatakiwa kulipa fedha hizo kwa haraka kama fidia ya madhara yaliyopatikana kwa mlalamikaji.

Inadaiwa kuwa  Septemba 6, 2016 maeneo ya Buguruni Sheli wilayani Ilala aliiba cheni  ya dhahabu gramu 38  yenye thamani sh. 60,000 kibangili ya mkononi n ash. 331,000 pamoja na pochi vyote thamani sh. 476,000, mali ya Mrisho.

Pia inadaiwa  kabla ya wizi huo alimchoma na kisu tumboni mgongoni na machoni ili kujipatia mali hiyo.

About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search