Kamishna Kichere amsimamisha kazi meneja TRA Mara...soma habari kamili na matukio360...#share


Na mwandishi wetu, Mara

Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA),  Charles Kichere amemsimamisha kazi Meneja wa TRA Mkoa wa Mara  Nicodemus Mwakilembe kwa kushindwa kusimamia vizuri mashine za  Kielektroniki za Kutolea Risiti (EFDs).


Charles Kichere

Uamuzi huo umetokana na ziara ya kushtukiza ya kukagua matumizi ya EFD aliyoifanya Kamshina Mkuu wa Tra kwenye baadhi ya maduka ya biashara Wilayani Bunda Mkoa wa Mara.

Akizungumza mara baada ya ziara yake, Kamishna Mkuu Kichere alisema kuna wafanyabishara wengi mkoani Mara  ambao walishalipa fedha kwa ajili ya kupata mashine za EFD lakini mpaka sasa hawajapatiwa mashine hizo.

"Katika ziara yangu nimegundua kwamba, wapo wafanyabiashara ambao wameshalipia mashine tangu mwaka 2013, 2014 na 2015 lakini mpaka sasa bado hawajapatiwa mashine za EFD na wamekuwa wakitumia mwanya huo kama kinga ya kutochukuliwa adhabu na TRA wakati Meneja wa Mkoa  yupo na hachukui hatua zozote. Huu ni uzembe uliopitiliza na kamwe siwezi kuuvumilia," amesema  Kichere.

Kichere amewaagiza mameneja wote wa TRA nchi nzima pamoja na majukumu mengine, kuhakikisha wanasimamia kikamilifu matumizi ya mashine za EFD katika mikoa yao na amesema hatasita kumuwajibisha meneja yeyote atakayeshindwa kutekeleza majukumu yake ipasavyo.

Ziara hiyo ya kushtukiza imewawezesha wafanyabiashara waliokuwa wamelipia mashine za EFD miaka ya nyuma, kupata mashine hizo na kufundishwa jinsi ya kuzitumia ambapo wengine wamejitokeza kununua mashine hizo kwa ajili ya biashara zao.

Kamishna  Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania yuko mkoani Mara kwa ziara ya siku tano  ambapo amepata nafasi ya kutembelea Vituo vya Forodha mipakani na ofisi mbalimbali za mamlaka hiyo pamoja na baadhi ya wafanyabiashara akikagua matumizi ya mashine za EFD.

About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search