Polisi kumchunguza Freeman Mbowe...soma habari kamili na matukio360...#share

Na Abraham Ntambara, Dar es Salaam

JESHI la Polisi Mkoa wa Kipolisi Kinondoni limesema litamchunguza mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe kuhusu kalituhumu jeshi hilo kuhusika na mashambulizi dhidi ya viongozi chama hicho.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Kinondoni ACP Muliro Muliro, akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.

Jana Mbowe alitoa shutuma za kutekwa, kuuwawa na watu wasiojulikana kwa katibu wa Chadema Kata ya Hananasifu jimbo la Kinondoni, Daniel John na mwili wake kutupwa kando ya fukwe za Coco beach.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa huo ACP Muliro Muliro ametoa msimamo huo leo alipokuwa akijibu swali la mwandishi aliyetaka kujua kauli ya jeshi hilo kuhusu tuhuma za Mbowe.

Pia alikuwa  akizungumza na waandishi wa habari  jinsi walivyojipanga kuelekea uchaguzi mdogo wa ubunge Kinondoni.

“…Tutachunguza kauli yake ili kujua anazungumza kwa misingi ipi na kipi kinamsukuma kutoa kauli hizo, hatuwezi kuacha mtu azungumze kwa hisia zake,” amesema ACP Muliro.

Amesema jeshi hilo lina taratibu za kufanya kazi zake na kwamba haliwezi kuburuzwa na hisia za mtu na kwamba tukio hilo wanaendelea kulifanyia uchunguzi ili kubaini waliohusika na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria.

ACP Muliro ameongeza kuwa Mbowe amekuwa akitoa mara kwa mara kauli za namna hiyo na kwamba kumekuwepo na hisia kama hizo dhidi yao lakini wanapokamilisha uchunguzi na kubaini ukweli watu huondoa hisia hizo ambapo aliwataka wananchi kutulia na kusubiri uchunguzi ukamilike.

Kuhusu uchaguzi wa marudi ubunge kinondoni
Amesema katika uchaguzi huo utakaofanyika Februali 17, 2018 jeshi hilo limejipanga kuhakikisha mchakato wote wa masuala ya uchaguzi unafanyika katika misingi ya sheria, kanuni na taratibu za uchaguzi.

Amewataka wananchi wa mkoa wa Kinondoni kujitokeza kwa wingi siku hiyo ili waweze kutekeleza haki yao ya kikatiba kwa kufuata sheria na taratibu watakazoelekezwa siku hiyo na wahusika wa uchaguzi bila kuleta vurugu au wao kuwa chanzo cha vurugu.

“Jeshi halitasita kuchukua hatua za haraka za kisheria kwa mtu yeyote au kikundi chochote chenye nia ya kupanga vitendo vya hujuma dhidi ya uchaguzi huo au kufanya vitendo vyovyote ambavyo ni kinyume na kanuni au sheria ya uchaguzi,” amesema.

Kuhusu kukutwa kwa mwili Coco beach.
ACP Muliro amesema jana majira ya asubuhi jeshi hilo kupitia kituo chake cha polisi Osterbay kilipokea taarifa kutoka kwa msamaria aliyekuwa katika shughuli zake maeneo ya fukwe za coco beach kuwa aliona mwili wa mtu akiwa kando ya bahari ya hindi.

Amesema baada ya kupata taarifa hiyo askari walikwenda eneo la tukio na kukuta mwili wa mtu mwenye jinsi ya kiume anayakadiriwa kuwa na umri kati ya miaka 30 hadi 35 ukiwa na majeraha kichwani, usoni, mkononi na miguuni, yanayoashiria kuwa amepigwa na kitu chenye ncha kali.

“Mwili huo ulichukuliwa na kupelekwa hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) ambapo madaktari walibaini kuwa mtu huyo tayari alikuwa amekwisha fariki, jalada la kuhusiana na kifo cha mtu huyo lilifunguliwa na uchunguzi ulianza mara moja ili kubaini chanzo cha kifo chake,” amesema.

Kuhusu kuvamia ofisi za chadema
Amekanusha jeshi hilo kuvamia ofisi za Chadema Magomeni na kwamba shutuma za namna hiyo dhidi yao ni za kifedhuli, kukejeli na kulidharirisha jeshi la polisi na kwamba walichofanya siku hiyo walirusha mabomu manne ya machozi kutawanya kikundi cha watu zaidi ya 100 waliokuwa wakifanya maandamano.


About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search