TRL yapata hasara bilioni 5.....soma habari kamili na matukio360....#share
Na Mwandishi Wetu, Morogoro
SHIRIKA la Reli Tanzania (TRL)
limepata hasara ya takribani shilingi bilioni tano katika kipindi cha mwezi
mmoja baada ya njia ya reli ya kati kusombwa na mafuriko katika Wilaya ya
Kilosa mkoani Morogoro na Gulwe mkoani Dodoma.
Waziri wa
Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa, akishiriki katika kazi
za kujaza mchanga kwenye viroba vinavyotumika kama kingo za kudhibiti maji ya
mto Mkondoa yasifike kwenye miundombinu ya reli katika eneo la kilosa, mkoani
Morogoro.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Ujenzi,
Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa wakati wa ziara ya kukagua
maendeleo ya ukarabati wa miundombinu ya reli hiyo na kusema kuwa Serikali
imejipanga kupata suluhisho la kudumu la uharibifu katika maeneo hayo ambapo
mara kadhaa yamekuwa yakiathiriwa na mvua kutokana na mabwawa yaliyopo kujaa
mchanga na hivyo kusababisha uharibifu huo.
“Serikali kwa sasa inayafanyia
kazi mapendekezo matatu yaliyowasilishwa na RAHCO ikiwemo kuihamisha reli
kwenye milima jirani, kuihamishia eneo ambapo inajengwa reli ya kisasa ya
SGR ama kujenga tuta kubwa, huku tukizingatia gharama halisi za kazi hiyo kabla
ya kufanya maamuzi", amesema Prof. Mbarawa.
Ameongeza kuwa mbali na Serikali
kuja na suluhu ya muda mfupi ya kurejesha safari za treni pia amewatoa hofu
wafanya biashara kwa kuwahakikishia kuwa mizigo yao iko salama na itasafirishwa
kwa wakati.
Kwa Upande wake Mkuu wa Mkoa wa
Morogoro, Dk. Steven Kebwe, amemuhakikishia Waziri Prof. Mbarawa kuwa Mkoa
umejipanga kuhakikisha unatoa elimu kwa wananchi kwenye utunzaji wa mazingira
ili kunusuru uharibifu unaotokea kutokana na shughuli za kibinadamu.
“Kama Mkoa tumejipanga kuwa kuanzia
sasa Sheria zilizopo zinazokataza kulima kandokando ya mito na kando ya reli
sasa zitafuatwa na tutaendelea kutoa elimu kwa wananchi ili miudombinu
hiyo isiathirike kwa sababu ya shughuli za kibinadamu zinazofanywa kupitia
kilimo", amesisitiza Dkt. Steven Kebwe.
Ameongeza kuwa kuanzia mwakani mkoa
umejipanga kutenga fedha kwa ajili ya kutumia njia za asili kulinda miundombinu
hiyo kwa kupanda miti na kuotesha matete ili kulinda miundombinu.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni
Hodhi ya Rasilimali za Reli (RAHCO), Massanja Kadogosa, amesema kazi ya
ukarabati imekamilika kwa sehemu kubwa kwani tayari treni tano za mizigo
zimepita salama na kuongeza kuwa kazi zinazomaliziwa kwa sasa ni kujaza mchanga
kwenye matuta ya reli hiyo na kumalizia kingo ili kuilinda reli.
No comments:
Post a Comment