Ujenzi barabara lami Kidatu-Ifakara waanza....soma habari kamili na matukio360....#share
Na
Mwandishi Wetu, Morogoro
SERIKALI imeanza ujenzi wa
barabara ya Kidatu-Ifakara yenye urefu wa km 66.9 kwa kiwango cha lami, kukamilika kwake kutachochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika wilaya za mkoa
wa Morogoro.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa
Makame Mbarawa (kushoto), akizungumza jambo na Mkuu wa Wilaya ya Kilombero,
James Ihunyo (kulia), katika ziara yake ya kikazi wilayani humo, mkoani Morogoro.
Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa
Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, alipokuwa akikagua
maandalizi ya ujenzi wa barabara hiyo na amemuagiza mkandarasi wa kampuni
ya Reynolds Construction kutoka Nigeria anayejenga barabara hiyo kujenga kwa
viwango na kukamilisha kwa wakati.
"Mradi huu umesuburiwa kwa siku
nyingi na wananchi wa wilaya hii na mkoa kiujumla, mategemeo ya Serikali ni
kuwa mradi huu utakamilika mapema mwezi Aprili, 2020 kwa kuzingatia
vipengele vya mkataba na kwa viwango stahiki", amesema Prof. Mbarawa.
Amesema ujenzi katika
barabara hiyo unatarajiwa kuhusisha ujenzi wa madaraja makubwa mawili,
madaraja madogo manne, makalavati makubwa na madogo 271 na unatarajiwa kudumu
kwa miaka 20.
Prof Mbarawa amesisitiza Serikali itahakikisha wananchi wa mkoa huo wanapewa kipaumbele kwenye ajira
mara tu kazi itakapoanza ili kuongeza kipato chao.
"Mradi umeanza na nimemuelekeza
mkandarasi kuajiri afisa mwajiri ili kuhakikisha nafasi nyingi za ajira
zinapatikana kwa wazawa kwani nafasi 70 walizoajiri mpaka sasa ni za mwanzo
tu, ila nafasi nyingine zitaongezwa", amefafanua Prof. Mbarawa.
Mkuu wa Wilaya ya
Kilombero, James Ihunyo, ameipongeza Serikali kwa jitihada inazozifanya
kuboresha miundombinu ya barabara nchini na amemuahidi Waziri Prof.
Mbarawa kuwa wananchi na uongozi wa usalama wa Wilaya yake watatoa ushirikiano
kwa mkandarasi huyo ili waweze kunufaika na mradi huo mapema.
Naye Meneja wa Wakala wa Barabara
(TANROADS), mkoa wa Morogoro, Mhandisi Dorothy Ntenga, amesema kuwa kazi halisi
itaanza mwishoni mwa mwezi Februari mwaka huu na watahakikisha wanamsimamia
mkandarasi kwa karibu ili ujenzi huo ukamilike kwa wakati na viwango.
Ujenzi wa barabara ya Kidatu-Ifakara
KM 66.9 kwa kiwango cha lami unatarajiwa kujengwa kwa miezi 30 na utagharimu
kiasi cha shilingi bilioni 111.4 na unafadhiliwa kwa ushirikiano wa Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jumuiya ya Umoja wa Ulaya (European Union),
Shirika la Misaada la Uingereza (UK aid) na Shirika la Misaada la Marekani
(USAID).
No comments:
Post a Comment