Waziri Mbarawa aipa TAA wiki mbili....soma habari kamili na matukio360...#share


Na Mwandishi Wetu, Mwanza

WAZIRI wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa ametoa wiki mbili kwa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Nchini (TAA), kukusanya fedha za madeni ambayo inadai kutoka kwa watoa huduma mbalimbali katika viwanja vyote vya ndege ili ziweze kutumika kuendeleza miundombinu.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa, akitoa maelekezo kwa Meneja wa Kiwanja cha Ndege Mwanza, Easter Madale (kushoto), alipokagua maendeleo ya upanuzi wa kiwanja hicho mkoani Mwanza.

Kauli hiyo ametoa jijini Mwanza, baada kukagua maendeleo ya upanuzi wa kiwanja cha ndege na hali ya uendeshaji katika kiwanja hicho ambapo amebaini kuwa kuna madeni ambayo yanaweza kulipika na kuweza kurahisisha shughuli za kiuendeshaji ikiwemo kujenga uzio ili kuongeza usalama kiwanjani hapo.

"Nataka TAA mkusanye madeni yote mnayodai, fedha hizi zikipatikana zinaweza kutumika kujenga uzio kwa ajili ya kulinda usalama wa uwanja ili wananchi wasiweze kuvamia na pia usalama wa ndege zinazoruka na kutua", amesisitiza Prof. Mbarawa.

Amefafanua kuwa kama Taasisi hizi zikikusanya madeni na watoa huduma wakalipa kodi kwa wakati kutasaida Serikali kuboresha maendeleo ya miundombinu.

Kuhusu maendeleo ya upanuzi wa kiwanja hicho. Prof. Mbarawa amesema ameridhishwa na kasi ya ujenzi ambapo kwa sasa umefikia asilimia 60.

Ameongeza kuwa ujenzi huo unategemewa kumalizika mwezi Julai mwaka huu na utagharimu kiasi cha shilingi takribani bilioni 94.

Aidha amesema Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa jengo la abiria mara miradi inayoendelea kukamilika.

Naye Msimamizi wa Kiwanja hicho ambaye ni Kaimu Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoa wa Mwanza, Mhandisi Joseph Mwami,  amesema kazi zinazoendelea kwa sasa ni pamoja na ujenzi wa jengo la kuongoza ndege, eneo la maegesho na njia za kuruka na kutua ndege

Mhandisi Mwami, amefafanua kuwa njia ya kuruka na kutua ndege katika kiwanja hicho imeongezwa urefu wa mita 500 ili kuifanya kufikia urefu wa KM 3.5 ili kuwezesha ndege kubwa za kimataifa kuweza kutua na kuruka katika kiwanja hicho.

Katika hatua nyingine Waziri Prof Mbarawa amekagua na kuridhishwa na ujenzi wa barabara ya Mwaloni-Pasiansi-Airport yenye urefu wa KM 5.3 kwa kiwango cha lami ambapo ujenzi wake umefikia zaidi ya asilimia 70 na unatarajiwa kukamilika mwezi mei mwaka huu na utagharimu kiasi cha shillingi bilioni 9.5.

"Nimekagua na niwapongeze Kampuni ya wazawa ya Nyanza Road kwa kazi nzuri mliyofanya katika ujenzi kwa barabara hii", amesema Prof Mbarawa.

Waziri Prof. Mbarawa ametoa wito kwa wananchi kutunza na kulinda miundombinu hiyo kwa manufaa ya kuongeza tija na maendeleo kwao kwan inapunguza msongamano wa magari kwa kiasi kikubwa na Serikali imekuwa ikitumia fedha nyingi kugharamia utekelezaji wa miradi hiyo.

Waziri Prof Mbarawa yuko mkoani mwanza kwa ziara ya siku akiwa na lengo la kukagua utekelezaji wa miundombinu ya sekta ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano


About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search