BMT yaingilia sakata kufungiwa maisha Wambura...soma habari kamili na matukio360...#share
Na Mwandishi Wetu, Dar es
Salaam
SIKU chache baada ya Makamu wa
Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Michael Wambura kufungiwa maisha
kujihusisha na masuala ya soka na Kamati ya Maadili ya shirikisho hilo,
Serikali imetaka maelezo ya sakata hilo zima.
Michael Wambura.
Kamati ya Maadili ya TFF ilimfungia
Wambura hivi karibuni baada ya Sekretarieti ya TFF kumshtaki kwenye kamati hiyo
kwa makosa matatu ya kimaadili ambayo ni kupokea pesa za TFF isivyo halali,
kugushi na kushusha hadhi ya TFF.
Katibu Mkuu wa Baraza la
Michezo la Taifa, (BMT) Mohammed Kiganja akizungumza leo na kituo kimoja cha
redio nchini, amesema wamelipa shirikisho hilo barua ikitaka ufafanuzi wa
sakata zima la Wambura pamoja na mchakato wa ajira ya Kaimu Katibu Mkuu wa TFF,
Wilfred Kidao.
“Ni kweli tuliomba maelezo ya
kufungiwa kwake, kwani tunaona kikao kilikaliwa tu siku moja na kutolewa
uamuzi,” amesema Kiganja.
Rais wa TFF, Wallace Karia
alikiri kupokea barua ya Wizara ya Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo ikitaka
maelezo juu ya suala la kufungiwa maisha kwa makamu wa rais huyo wa TFF.
Karia alisema, taarifa hizo
hazitaishia Wizarani bali watazipeleka hata Shirikisho la Soka Afrika, CAF na
lile la Kimataifa, (Fifa).
“Ni kweli Wizara ilituuliza juu
ya suala hilo, tumewajibu namna lilivyokuwa hadi kusimamishwa Wambura,” alisema
Karia.
Habari zaidi kutoka TFF
zimelidokeza Mwananchi kuwa, Serikali ilipinga mchakato uliotumika kumsimamisha
Wambura na kutompa nafasi ya kumsikiliza hata kama amekosea na ndiyo maana
ilitaka maelezo hayo.
“Ilichokitaka Serikali ni
kufahamu kama utaratibu mzima wa kumsimamisha Wambura ulifuatwa na ilisema kama
kakosea bado alikuwa na haki ya kusikilizwa,”
Mbali na hayo, Kifungu cha tano
(d) cha ibara ya 31 ya Katiba ya TFF, inayofafanua juu ya muundo wa Kamati ya
Utendaji, kinazuia mjumbe yeyote wa Kamati ya Utendaji ya Shirikisho hilo
kung’olewa kwenye nafasi yake kwa makosa ya jinai ambayo hayajathibitishwa.
Hata hivyo, Karia alisema jana
kwamba Wambura atasikilizwa kwani ni haki yake na tayari amekata rufaa kupinga
hukumu yake.
Wakati hayo yakiendelea,
Mwananchi limedokezwa kuwa, mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya TFF, Athuman
Nyamlani ndiye anapigiwa chapuo la ‘kuvaa viatu’ vya Wambura TFF.
Chanzo hicho cha kuaminika
kilidokeza kuwa, pamoja na mpango huo, Serikali imeiwekea ngumu TFF katika
mchakato huo ikitaka utaratibu ufuatwe.
Hata hivyo, Karia alisisitiza
kuwa mrithi wa Wambura TFF atapatikana kwa kuchaguliwa kwenye uchaguzi mdogo
utakaopangwa baadaye.
Kuhusu suala la Kidau, Serikali
pia imetaka maelezo ya hili na Rais Karia alisema wako kwenye mstari na
hawajavunja Katiba ya TFF kwenye mchakato wa kumpata mtu wa nafasi hiyo.
Inaelezwa kuwa Kidau ni Mjumbe
wa Kamati ya Utendaji ya TFF kupitia Tafca kabla ya kuteuliwa kuwa kaimu katibu
mkuu hatua inayoelezwa kuwa ni kinyume na Katiba ya TFF.
Katiba ya TFF kifungu cha 41
(3) kinasema waajiriwa wa TFF akiwemo katibu mkuu hatakiwi kuwa mjumbe wa
chombo chochote ndani ya TFF kwa, aidha kuteuliwa au kuchaguliwa.
“Taarifa za kukiukwa Katiba
zinaenezwa na baadhi ya watu, lakini TFF haijakiuka kwani Kidau kwanza
hajaajiriwa TFF tumemuomba tu akaimu, lakini tayari alishaachia ngazi Tafca,”
alisema Karia.
Alisema hata ikitokea Kadau
akawa Katibu Mkuu wa TFF, bado hawajavunja Katiba ya TFF kwa kuwa si Mwenyekiti
wa Tafca kwa sasa.
No comments:
Post a Comment