Dk. Nchemba alitaka jeshi la polisi kuwasweka rumande madereva wanaosababisha ajali...soma habari kamili na matukio360...#share
Na Lilian Lundo - MAELEZO, Dodoma
Waziri
wa Mambo ya Ndani ya Nchi Dk. Mwigulu Nchemba amelitaka Jeshi la Polisi
kuwaweka ndani madereva wanaosababisha ajali kutokana na mwendo kasi na baadaye
kupelekwa Mahakamani.
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Mwigulu Nchemba akijibu hoja mbalimbali za wabunge wakati wa Mkutano wa Kumi na Moja wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, leo Mjini Dodoma.
Dk. Nchemba
ametoa agizo hilo leo Bungeni Mjini Dodoma alipokuwa akijibu muongozo wa Mbunge
wa Ulanga Morogoro Mhe. Goodluck Mlinga, juu ya chanzo cha ajali ya basi la
City Boy kutoka Karagwe Mkoani Bukoba kuelekea Dar es Salaam ambalo liligongana
uso kwa uso na lori aina ya Fuso lililokuwa linatoka Singida kuelekea Igunga
usiku wa Aprili 04 mwaka huu na kusababisha vifo vya watu 12.
"Hatuwezi
kuacha watu wanapotea kwa ajili ya uzembe wa mtu mmoja na kuleta hasara na
vilio vikubwa kwa Watanzania," alisema Dk. Nchemba.
Amesema,
ajali nyingi zinazotokea hapa nchini zinasabishwa na mwendokasi na sio tatizo
la miundombinu ambapo katika ajali zilizoripotiwa ajali 1500 zilisababishwa na
mwendo kasi na ajali 89 zimetokana na miundombinu.
Aidha Dk.
Nchemba amesema, Tanzania ni moja ya nchi zenye barabara bora hivyo ajali
nyingi zinazotokea husababishwa na uzembe wa madereva pamoja na mwendokasi.
Wakati
huohuo bungeni hapo, Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce
Ndalichako amesema Serikali imeweka utaratibu mashuleni wa kuwawezesha watoto
wa kike kuripoti matukio ya udhalilishaji na pia imeanzisha klabu mbalimbali za
kuwajenge uwezo na ujasiri wa kuweza kuripoti matukio ya udhalilishaji.
Hata
hivyo Prof. Ndalichako amewataka watoto kutokuwa na uwoga wowote kwa sababu
Serikali yao inawalinda, hivyo pale wanapofanyiwa vitendo kinyume na matakwa ya
Serikali watoe taarifa ili Serikali ichukue hatua stahiki kwa wale wote wanao
wadhalilisha na kusababisha watoto wasisome kwa amani.
No comments:
Post a Comment