Halima Mdee kufikishwa mahakamani Jumanne...soma habari kamili na matukio360...#share
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
MBUNGE wa Kawe Chadema, Halima Mdee, anatarajia kufikishwa mahakamani Jumanne Aprili 3.
Halima Mdee, Mbunge Kawe
Mdee atakuwa akiungana na viongozi wengine wa Chama hicho akiwamo Mwenyekiti wake Freeman Mbowe, wanaoshtakiwa kwa makosa manane yakiwamo uchochezi, kuhamasisha maandamano na uasi.
Akizungumza leo Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, SACP Lazaro Mambosasa amesema kuwa mbunge huyo amekiuka masharti yaliyomtaka kuripoti kituo cha polisi pamoja na viongozi wengine saba wa chama hicho kabla ya kufikishwa mahakamani.
"Kosa lake ni kukiuka masharti ya yaliyomtaka kuripoti kituo cha polisi na wenzake kabla ya kufikishwa mahakamani," amesema SACP Mambosasa.
Halima alikamatwa leo Jumapili Aprili Mosi, saa tisa alfajiri katika Uwanja wa Ndege wa Mwalimu Julius Nyerere (JNIA), alipokuwa akirejea nchini akitokea Afrika Kusini alipokuwa akipatiwa matibabu.
Aidha, alipoulizwa ni kwanini Halima amekamatwa wakati mawakili wake walikuwa wakitoa taarifa zake, Mambosasa amesema: “hayo ni maneno tu, anafahamu taratibu zikoje, anafahamau sheria zinasemaje kwa sababu wanatunga wenyewe huko bungeni hilo si suala la kujadili na mimi, asubiri atajibu hayo mahakamani.
Mambosasa amesema hayo muda mchache baada ya Chadema kulitaka Jeshi la Polisi kumpatia dhamana Mbunge ili aweze kuendelea na matibabu.
Mkurugenzi wa Itifaki, Mawasiliano na Mambo ya Nje ya chama hicho, John Mrema amesema licha ya kwamba Mbunge huyo kuwa mgonjwa ambaye hivi punde ametoka hospitali, lakini pia dhamana ni haki yake na lawama zote zitakuwa juu yao endapo afya ya mbunge huyo itatetereka.
“Hadi mchana wa leo Aprili Mosi, Jeshi la Polisi limeendelea kumshikilia Katika Kituo Kikuu cha Polisi Dar es Salaam na hajapatiwa dhamana pamoja na daktari wake kuwathibitishia polisi kuwa Mheshimiwa Halima ni mgonjwa.
“Tunasikitishwa na kulaani kitendo hiki cha polisi kuendelea, kumshikilia mgonjwa ambaye alikuwa amelazwa hospitalini, , tumetuma mawakili daktari wake lakini hawajafanikiwa mwisho, Jeshi la Polisi litawajibika kwa Watanzania endapo afya ya Halima Mdee ikitetereka au ikidhoofu zaidi na lawama zote zitakuwa juu yao,” amesema Mrema




No comments:
Post a Comment