Watumishi wa sekta ya ujenzi watakiwa kujitathimini...soma habari kamili na matukio360...#share
Na Mwandishi Wetu, Morogoro
WAZIRI wa Ujenzi, Uchukuzi na
Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa, amewataka wajumbe wa baraza la wafanyakazi
wa Sekta ya Ujenzi kujitathimini yale waliyoazimia kutekeleza kwa mwaka wa
Fedha 2017/18 kama yamefikia lengo ili kuweza kusaidia kuboresha utendaji na
kutafutia ufumbuzi masuala ambayo yanakwamisha ufanisi wa kazi na kuwezesha
mazingira wezeshi kwa wafanyakazi.
Waziri wa Ujenzi,
Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa, akizungumza na wajumbe wa baraza
la wafanyakazi wa Sekta ya Ujenzi (hawapo pichani), wakati wa ufunguzi wa
baraza hilo lililofanyika mkoani Morogoro.
Prof. Mbarawa amesema hayo mkoani
Morogoro, wakati akifungua kikao cha baraza la wafanyakazi ambapo pamoja na
mambo mengime amesisitiza umuhimu wa baraza hilo katika kuhakikisha kuwa
waajiri na watumishi wanatambua wajibu na haki zao kwa kuzingatia maadili ya
utumishi wa umma ili kuleta matokeo chanya katika utendaji kazi wenye tija,
staha na upendo.
"Ni matarajio yangu kuwa kila mjumbe
kwa nafasi aliyonayo katika baraza hili atatumia fursa hii kutoa michango ya mawazo
ili iweze kuwa mwongozo mzuri wa kutekeleza majukumu kwa ufanisi", amesema
Prof. Mbarawa.
Aidha, ametoa wito kwa wajumbe hao
kuhakikisha kuwa Wizara inashiriki kikamilifu katika kutekeleza azma ya
Serikali ya kuwajengea watanzania miundombinu bora na imara ili kuifanya
Tanzania iwe nchi ya viwanda na hivyo kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya
Maendeleo ya kuifanya nchi yetu iwe na uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.
Profesa Mbarawa, amewataka wajumbe hao
kujadili kwa kina Rasimu ya Bajeti na Mpango wa utekelezaji kwa mwaka wa fedha
2018/19 ili kuweza kuleta tija na ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya
Wizara.
Awali akimkaribisha mgeni rasmi
Waziri Prof. Mbarawa, Mwenyekiti wa baraza hilo ambaye ni Katibu Mkuu wa Sekta
ya Ujenzi Mhandisi Joseph Nyamhanga, amesema kuwa mabaraza ya wafanyakazi
yameanzishwa kwa madhumuni ya kuishauri Serikali katika ngazi ya Wizara, Idara
na Taasisi za Umma kuhusu usimamizi wa rasilimali watu, utekelezaji wa majukumu
kwa ufanisi na weledi kwa kuzingatia sheria, kanuni na maadili ya utumishi wa
umma.
Ameongeza majukumu mengine kuwa ni
kulinda haki na wajibu wa waajiri na wafanyakazi; kutoa ushauri kuhusu kujenga
hali bora za kazi; maslahi ya Wanyakazi na kusimamia haki na ustawi katika
sehemu za kazi.
No comments:
Post a Comment