TIC yawataka watanzania kuchangamkia fursa ujio wawekezaji nchini..soma habari kamili na matukio360...#share


Na Abraham Ntambara, Dar es Salaam

KITUO cha Uwekezaji nchini (TIC) kimewataka watanzania kuchangamkia fursa ya ujio wa wawekezaji katika kujinufaisha kiuchumi na ukuaji wa viwanda kwa kushirikiana nao kibiashara.

Bw. Geoffrey Mwambe (wa pili kutoka kulia) akiinadi Tanzania  kwenye jipo la wataalamu wa uchumi walioongoza mjadala wa upatikanaji wa mitaji, mazingira na fursa za uwekezaji ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki wakati wa kongamano la Ujerumani na Afrika Masghariki, Berlin.

Hayo yamesemwa na leo jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mtendaji Kituo hicho  Geofrey Mwambe wakati akizungumza na waandishi wa habari akitoa taarifa kuhusiana na ziara aliyofanya ya kikazi nchini Ujerumani na Uholanzi kati ya tarehe 14 mpaka 17, Mei 2018 ikiwa ni jitihada zake za kutangaza fursa za uwekezaji  ili kushawishi na kuvutia wawekezaji kuja kuwekeza nchini.  

“Ni vyema wawekezaji wa hapa nchini wakajenga uhusiano mzuri na wawekezaji kutoka nje ya nchi kwani ni jambo ambalo litasaidia kuendelea kukuza maendeleo ya uchumi wa viwanda,” amesema Mwambe.

Amesema watanzania wanatakiwa kujitokeza kwa wingi kujiunga na wawekezaji kutoka nje ili waweze kupata uelewa wa kutosha katika ufanyaji wa biashara wa kimataifa lakini pia kufahamu mtu ambaye wanataka kufanya naye biashara.

Mwambe amesema pamoja na kutokuwa na mitaji ya kutosha, amewataka baadhi ya watanzania kuepukana na dhana ya kuwa wawekezaji ni kutoka nje ya nchi pekee bali nao wanapaswa kuwekeza kwa kutumia fursa zilizopo kwani mazingira ya uwekezaji ni mazuri.

Hapa chini ni taarifa kamili za Ziara ya Mkurugenzi Mtendaji wa TIC Geofrey Mwambe katika nchi za Ujerumani na Uholanzi.

MKURUGENZI Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) Bw. Geoffrey Mwambe amefanya ziara ya kikazi nchini Ujerumani na Uholanzi kati ya tarehe 14 mpaka 17, Mei 2018 katika jitihada zake za kutangaza fursa za uwekezaji  ili kushawishi na kuvutia wawekezaji kuja kuwekeza nchini.  

Akiwa nchini Ujerumani Bw. Mwambe alipokelewa na Balozi wa Tanzania nchini Ujerumani Mhe. Dkt. Possi Abdallah ambapo walifanya kikao cha kazi kabla ya kushiriki kongamano la biashara na uwekezaji kati ya Ujerumani na nchi za Afrika Mashariki lililofanyika Mei 15, 2018 katika mji wa Berlin. Kongamano liliandaliwa ili kutoa nafasi kwa nchi za ukanda wa Afrika Mashariki kunadi fursa za uwekezaji kwa wafanyabiashara wa Ujerumani na dunia kwa ujumla.


Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji  Tanzania Bw. Geoffrey Mwambe (kulia) alipomtembelea  Balozi wa Tanzania nchini Ujerumani Mhe. Dkt. Possi Abdallah ofisini kwake Berlin, Ujeruman.
                              
Vilevile siku mbili baada ya kongamano, Kituo kilifanya ziara nchini Uholanzi ambapo kilifanikiwa kusaini makubaliano ya mashirikiano (MOC) na Taasisi ya Biashara za Kimataifa ya Uholanzi (DCIB) pamoja na kufanya mkutano na baadhi ya wafanyabiashara wa Taifa hilo wenye nia ya kuja kuwekeza nchini. Sekta zitakazohusika ni pamoja na mafuta, gesi, kilimo, afya, usafirishaji, viwanda, fedha, mazingira, nishati na mawasiliano.

Pichani  baada ya kukamilisha zoezi la kusaini MOC . waliokaa kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa TIC Bw. Geoffrey Mwambe na kushoto ni Mwenyekiti wa DCIB Bw. Hans Biesheuvel. Pamoja nao kulia ni Mkurugenzi wa Uhamasishaji Uwekezaji wa TIC Bw. John Mnali,Balozi wa Tanzania nchini Uholanzi Mhe. Irene Kasyanju,Mkurugenzi Mkuu wa DCIB Dkt Dewanand Mahadew na Bi Zeinab Dauda Meneja wa DCIB Afrika Mashariki.

Makubaliano yaliyomo kwenye MOC yatadumu kwa kipindi cha miaka mitano (5) na malengo yake ni:
i.                 I/ kubadilishana taarifa za fursa na mazingira ya uwekezaji
ii.       kuratibu ujio wa wafanyabiashara wa Uholanzi kuja Tanzania  kuwekeza na kufanya biashara na Watanzania kwenda Uholanzi
iii.         II/ kujengea uwezo Kituo cha Uwekezaji kufanya kazi zake za kutafiti, kuhamasisha na kufanikisha uwekezaji
iv.          III/ kukuza sekta binafasi ya Tanzania hususan wawekezaji wa ndani na wajasiriamali kupitia mafunzo mbalimbali.

Kupitia kongamano, Bw. Mwambe alielezea majukumu ya Kituo, msaada unaotolewa kwa wawekezaji katika kuanzisha miradi, hali ya uchumi na mikakati mbalimbali inavyotekelezwa na Serikali ya awamu ya tano chini ya uongozi mahiri wa Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli  kwa lengo la kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji ili kuvutia uwekezaji wa mitaji ya kutoka nje (FDI).

Akiainisha baadhi ya maeneo ambayo yanafanyiwa kazi na Serikali alisema ni pamoja  na kuweka mazingira wezeshi ya usajili wa biashara na leseni kwa wawekezaji wa ndani na nje pamoja na kuondoa urasimu ndani ya mifumo ya Serikali kuanzia ngazi ya Mtaa/Kijiji hadi Taifa ili kufanikisha utekelezaji wa miradi ya uwekezaji kwa muda mfupi.
  
Bw. Mwambe pia aliwahakikishia wawekezaji wa nchini Ujerumani na Dunia kwa ujumla kuwa Tanzania ni nchi yenye fursa nyingi na mahali salama kwa uwekezaji ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Afrika;  hivyo wawekezaji wenye mitaji na teknolojia wanakaribishwa kuja kuwekeza kwenye sekta mbalimbali  ambazo kwa sasa ni kipaumbele cha Taifa yaani viwanda, kilimo, madini, mifugo, uvuvi, miundombinu, uzalishaji na usambazaji umeme na miundombinu kwa ujumla.

Nae mwakilishi wa Benki ya Stanbic kwa Kanda ya Afrika Mashariki Bw. Jibran Qureishi alieleza kuwa kwa sasa Tanzania inafanya vizuri katika masuala ya Kiuchumi ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Afrika kwa ujumla. Matokeo hayo chanya ni kutokana na uongozi mahiri wa Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli aliyeanzisha vita ya kupambana na rushwa; na kupunguza urasimu kwa lengo la kuweka mazingira wezeshi ya uwekezaji.

Sehemu ya washiriki wa kongamano la Biashara na Uwekezani kati ya Ujerumani na Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki wakifuatilia mawasilisho ya mada ya juu ya hali ya uchumi kwa nchi za Afrika Mashariki

Bw. Qureishi ambaye ni mchumi mbobezi aliweka bayana kwamba Tanzania ina nafasi kubwa ya kuendelea kufanya vizuri zaidi katika nyanja ya uchumi kwa miaka ya hivi karibuni baada ya kukamilika kwa miradi mikubwa ya maendeleo inayotekelezwa  na Serikali kwa kutumia rasilimali za ndani na sio mikopo kama ilivyokuwa imezoeleka. 

Akitaja baadhi ya miradi hiyo ni mradi wa kuzalisha umeme wa Stiegler's Gorge, ujenzi wa reli ya kisasa kutoka Dar es salaam mpaka Dodoma na upanuzi wa bandari. Kwa ujumla ziara ya Kituo nchini Ujerumani na Uholanzi imekuwa ya manufaa yenye manufaa kwenye maeneo yafuatayo:-

Moja, kwa upande wa Ujerumani tumekutana na makampuni ambayo yameonesha nia ya kuwekeza kwenye sekta za viwanda, afya, ujenzi, miundombinu, mawasiliano, usafirishaji na nishati.

Pili, kuanza kwa utekelezaji wa makubaliano ya ushirikiano kati ya Kituo na Taasisi ya Biashara za Kimataifa ya Uholanzi kunatoa fursa ya kutekelezwa masuala mbalimbali kwenye miradi ya ubia, upatikanaji wa fedha za miradi, uhamishaji wa teknolojia na ujuzi, kuandaa semina /warsha na misafara ya wawekezaji. Kituo kinatarajia kupokea kundi la kwanza la wafanyabiashara kutoka Uholanzi mapema mwaka 2018/2019.

Tatu, kwa upande wa Uholanzi tumekutana na makampuni yaliyoonesha nia ya kuwekeza kwenye sekta za utalii, ujenzi wa kiwanda cha kutengeneza spea za magari, uanzishaji wa chuo cha mafunzo ya ufundi (Vocational Training), uanzishaji wa mradi wa usimamizi wa usalama wa mizigo kuanzia bandarini mpaka eneo husika na usimikaji wa mitambo ya kutengeneza bidhaa mbalimbali za ngano.

Mkurugenzi Mtendaji wa TIC Bw. Geoffrey Mwambe alipomtembelea Balozi wa Tanzania nchini Uholanzi, Mhe. Irene Kasyanju ofisini ,The Hague,  Uholanzi.

Kwa upande wake Balozi wa Tanzania nchini Uholanzi, Mhe. Irene Kasyanju amesema kusainiwa kwa makubaliano kati ya TIC na DCIB ni hatua kubwa ambayo itarahisisha utekelezaji wa sera, diplomasia ya uchumi. Mhe. Balozi amehitimisha kwa kuhimiza wadau wa sekta binafsi ya Tanzania kutumia vema makubaliano hayo kama fursa ya kuongeza biashara na uwekezaji kwa kushirikiana na wadau kutoka Uholanzi.

About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search