Mtambo wa Marekani kuzuia makombora ya Korea Kaskazini waanza kazi
![]() |
| Mtambo wa Thaad umewekwa kuzuia makombora kutoka Korea Kaskazini |
Jeshi la Marekani limesema mfumo wake wa Thaad wa kutoa kinga dhidi ya makombora umeanza kufanya kazi nchini Korea Kusini.
Msemaji wa jeshi hilo amesema mtambo huo sasa una uwezo wa kuzuia makombora yanayorushwa na Korea Kaskazini na pia kuilinda Korea Kusini.
Lakini maafisa wameambia wanahabari kwamba itachukua miezi kadha kabla ya mfumo huo katika kutumika kikamilifu.
Hali ya wasiwasi imekuwa ikitanga katika rasi ya Korea, huku Korea Kaskazini ikiendelea kutoa vitisho mara kwa mara.
Marekani nayo imetuma kundi la meli za kivita pamoja na nyambizi katika rasi hiyo.
Jumatatu, ndege mbili za kuangusha mabomu za Marekani zilifanya mazoezi ya pamoja na jeshi la wanahewa la Korea Kusini, operesheni ambayo Marekani ilisema ilikuwa ya kawaida.
Mtambo wa Thaad, ambao kwa kirefu husimamia Terminal High Altitude Area Defence, ulianza kuwekwa wiki iliyopita katika eneo ambalo zamani lilikuwa uwanja wa gofu katika eneo la Seongju katikati mwa Korea Kusini.
Baadhi ya raia wa Korea Kusini waliandamana kuupinga.
Wengi wa wenyeji wanaamini mtambo huo unaweza kulengwa na adui na hivyo kuhatarisha maisha ya watu wanaoishi hapo karibu.
China pia imepinga kuwepo kwa mtambo huo - ikisema uwezo wake wa rada huenda ukahitilafiana na operesheni zake za kijeshi.
Msemaji wa jeshi la Marekani aliyepo Korea Kusini alisema mtambo huo wa Thaad sasa "unafanya akzi na una uwezo wa kuzuia makombora yanayorushwa kutoka Korea Kaskazini na kuilinda Jamhuri ya Korea."
![]() |
| Baadhi ya wakazi Korea Kusini waliandamana kupinga kuwekwa kwa mtambo huo |
- bbc swahili





No comments:
Post a Comment