Upambe: ADC washangazwa na 'upambe' wa CHADEMA kwa Chama cha Wananchi CUF.. wakemea mauaji ya Kibiti... #share


CHAMA cha Alliance For Democratic Change (ADC), kimemuomba Rais John Magufuli kuachia vyama vya siasa vya upinzani kufanya shughuli za kisiasa kwa kuwa ni takwa la kisheria.




Kauli hiyo imetolewa jana jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu Taifa wa chama hicho, Doyo Doyo aliyesema hali ya kisiasa nchini si nzuri na kwamba Serikali kwa kuendelea kuzuia shughuli za kisiasa ni tishio kwa vyama kama ADC akisema huenda vikafa.

“Hali ya kisiasa sio nzuri sana, kuna hali ya kutopata uhuru wa kufanya siasa hasa katika upande wa vyama vya upinzani katika nchi yetu. Kuzuiwa kufanya mikutano ya kisiasa, makongamano na kadhalika, hii inaua vyama vya siasa,”alisema na kuongeza:

“ADC inamuomba Rais John Magufuli atuachie tufanye mikutano kwani jambo hili ni takwa la kisheria.”

Akizungumzia usalama nchini alisema hawaridhishwi na taarifa za mauaji yanayoendelea Kibiti mkoani Pwani akisema yanatia doa Taifa, ambapo aliiomba Serikali kujipanga upya na kuweka mkakati madhubuti ya kukabiliana na wahalifu.

Kuhusu migogoro ndani ya vyama vya siasa Doyo alisema ADC kinashangazwa na mgogoro wa Chama cha Wananchi (CUF) kushindwa kupatiwa ufumbuzi wa haraka hali inayofanya wanachama wake kuanza kukata tamaa.

Alisema ADC unachukizwa na hali hiyo kwani kuendelea kwa mgogoro huo kwa muda mrefu ni kunadhoofisha afya ya upinzani katika macho ya Watanzania.

“Nawaomba Maalim Seif Sharif Hamad na Profesa Ibrahim Lipumba wakae pamoja ili kumaliza tofauti zao,” alisema Doyo.

Aidha, alieleza kushtushwa kwa ADC na matamko mbalimbali ya viongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kuingilia mgogoro huo wa CUF.
Doyo aliwashauri Chadema kuacha mara moja kuingilia mgogoro usiowahusu akidai kitendo hicho cha kuingilia mgogoro huo usiowahusu ni mkakati wa kisiasa wa kujitengenezea hati miliki ya kisiasa nchini, lakini pia kinaweza kuhatarisha amani.

Hata hivyo, Doyo alisema alimpongeza Rais Magufuli kwa juhudi zake anazofanya kuzuia rasilimali za nchi hasa kwa kitendo cha kuwasilisha miswada kwa hati ya dharura bungeni ili kufanyiwa marekebisho ya sheria.

Na Abraham Ntambara




About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search