uPDATES: Lissu ahojiwa kwa makosa 2 polisi....Alala Mahabusu....Chadema watoa neno zito...#share
*Media updates from central*
Mwanasheria Mkuu wa CHADEMA Tundu Lissu amehojiwa kwa tuhuma
za kufanya makosa mawili;
1. Kumkashifu rais (kusema makosa ya rais hadharani).
2. Uchochezi kuhusu kuzuiliwa na kushikiliwa kwa ndege ya
serikali ya bombardier.
Makosa hayo yanadaiwa kufanywa kwenye mkutano na waandishi wa
habari uliofanyika Ijumaa iliyopita, Agosti 18, mwaka huu.
Lissu ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Singida Mashariki na
Mnadhimu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, amekataa kutoa maelezo yoyote
polisi, akitumia haki yake ya kisheria kuwa mtuhumiwa ana haki, kisheria,
kutaja jina na anuani yake tu anapokuwa anashikiliwa na polisi hadi
atakapopelekwa mahakamani ambako ndiko atataoa maelezo kujibu mashtaka
anayotuhumiwa nayo.
Lissu ambaye ameendelea kuwa imara akiwa tayari kujibu
mashtaka yake mahakamani, akiwa polisi amepata msaada wa kisheria kutoka kwa
Wakili Faraji Mangula, ambaye pia anashughulikia uwezekano wa mteja wake kupata
dhamana kwa mujibu wa sheria.
Chama kimeshatoa maelekezo kwa wanasheria wa chama kwa ajili
ya kuchukua hatua zaidi za kisheria iwapo Jeshi la Polisi halitampeleka mbele
ya mahakama Lissu ndani ya muda unaoagizwa na sheria za nchi yetu.
Aidha, chama kinaendelea kusisitiza kuwa serikali bado inao
wajibu wa kujibu hoja za msingi zilizotolewa na Chama kupitia tamko lililosomwa
na Mwanasheria Mkuu wa Chama Lissu kwenye mkutano na waandishi wa habari kuhusu
kushikiliwa kwa ndege ya Tanzania huko nchini Canada kwa sababu ya deni
tunalodaiwa kama nchi la shilingi bil. 87.
Tunaikumbusha serikali kuwa mojawapo ya hoja zilizotolewa na
chama katika tamko hilo ni pamoja na;
1. Kwanini Serikali, kupitia kwa Waziri wa Ujenzi wa wakati
huo, John Magufuli ilivunja mkataba wa Kampuni ya Stirling Civil Engeering Ltd?
Kitendo ambacho kimesababisha nchi yetu kuingizwa hasara kwa kudaiwa mabilioni
ya shilingi.
2. Kwanini deni la Stirling Civil Engeering Ltd halikulipwa
mara baada ya mahakama ya usuluhishi kutoa tuzo ya dola za Marekani mil. 25,
kitendo ambacho kimesababisha deni hilo sasa kufikia dola mil. 38.711?
3. Wananchi wanataka kujua katika kashfa hiyo ambayo ni
dhahiri inalitia doa na aibu kubwa taifa letu kuwa halizingatii sheria na
taratibu katika uendeshaji wa masuala yake, *NANI* atawajibika kijinai kwa
kulisababishia taifa letu hasara ya bilioni 87?
4. Je serikali hii ya CCM ambayo imekuwa ikijigamba kuwa inao
uwezo wa kutumbua majipu, je itaweza kutumbua hilo?
Leo ikiwa ni siku ya tano tangu CHADEMA kilipotoa hadharani
tamko hilo kuhusu kashfa hiyo ya kuzuiliwa kwa ndege hiyo ya Bombardier huko
Canada, Serikali haijajibu hoja zilizotajwa hapo juu kwa ukamilifu wake. Ni
vyema serikali ikatoa hadharani na majibu yenye hoja badala ya kutaka
kupindisha kwa kumkamata na kumshtaki Mwanasheria Mkuu wa Chama, Tundu Lissu
ambaye alisoma tamko hilo mbele ya viongozi wakuu wa chama kwa niaba ya
wanaCHADEMA nchi nzima.
*Tumain Makene, Ofisa Habari Chadema*




No comments:
Post a Comment