TGNP: ‘Mifumo kandamizi katika siasa yanyima wanawake fursa ya uongozi’...Rushwa ya Ngono yatajwa kutumika kuwapa wanawake uongozi ndani ya vyama na serikali....#share
MTANDAO wa Jinsia Tanzania (TGNP) umesema mifumo kandamizi iliyopo katika siasa unamnyima mwanamke
haki ya uongozi na ushiriki katika shughuli za kidemokrasia.
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TGNP, Vicensia Shule
(kushoto) akizungumza na waandishi wa habari leo kuzungumzia Tamasha la Jinsia
la mwaka 2017 linalotarajia kuanza rasmi Septemba 5 hadi 8 ya mwaka 2017 katika
viwanja vya TGNP Mabibo jijini Dar es Salaam.
Aidha umesema hali hiyo inasababisha uwepo wa idadi ndogo ya
wanawake katika nafasi za uongozi na maamuzi kuanzia serikali za mitaa hadi
serikali kuu, Bunge, Mahakama na nyadhifa nyingine.
Hayo yameelezwa leo jijini Dar es Salaam na Mwenyekiti wa
Bodi ya TGNP Vicensia Shule.
Akizungumza na waandishi wa habari juu ya Tamasha la Jinsia
la 14 la Siku Nne, litakalofanyika kuanzia kesho hadi Septemba 8 mwaka huu
lenye lengo la kujadili changamoto zinazomkabili mwanamke za kiuchumi, kisiasa na kijamii na jinsi ya
kuzitatua.
Amesema kuwa kikwazo hicho kinatokana na vyama kutokuwa na
miongozo ya viwango vya uwakilishi kwa jinsia huku akibainisha kuwa mfumo
uliopo na kwamba kila chama kina
utaratibu wake wa kupendekeza wagombea ambao mara nyingi unakosa uwazi na
unagubikwa na rushwa ya ngono.
“Mara nyingi wanawake na wasichana wamekuwa wakibaguliwa
kwenye sehemu za afya, elimu, uwakilishi wa kisiasa, soko laajira na
kwengineko. Hali hii inakuwa na athari hasi kwa maendeleo ya vipaji vyao na
uhuru wao wa kuchagua,” alisema Shule.
Akizungumzia kuhusu tamasha hilo, Shule amesema tamasha la mwaka
huu litalenga kujenga mikakati ya muda mrefu ya mageuzi ya mifumo hiyo
kandamizi.
Tamasha litakuwa na mada ndogo ndogo tatu ambazo ni uongozi
na maendeleo, haki ya kiuchumi kwa mwanamke na wanawake historia yetu.
Ametaja malengo makuu ya tamasha hilo kwa mwaka huu kuwa ni
kutafakari na kusherehekea mafanikio, changamoto zilizopo katika kuendeleza
usawa wa kijinsia, wakizingatia utekelezaji wa mikataba, maazimio, sera na
mikakati mbalimbali ya kimataifa, kikanda na kitaifa.
Mengine ni kutathimini ushiriki wa wanawake katika michakato
ya kufanya maamuzi katika uongozi wa kisiasa kwenye serikali za mitaaa.
Kufuatilia, kuhifadhi, kutambua na kusherehekea viongozi wanawake wenye
michango ya kuigwa juu ya usawa wa kijinsia na uwezo wa wanawake, hususani
mapambano dhidi ya mfumo dume na uliberali mamboleo.
Pia imo kuimarisha harakati za ukombozi wa wanawake
kimapinduzi kupitia ujenzi wa nguvu za pamoja.
Aidha Shule amesema pia wadau watapata kubadilishana uzoefu,
kujengeana uwezo, kutafakari na kusherehekea changamoto na mafanikio katika
kufikia usawa wa kijinsia.
Na Abraham Ntambara
No comments:
Post a Comment