JPM ampa mtihani Waziri Prof. Kabudi...Soma habari kamili na Matukio360.#share
RAIS
John Magufuli amemuagiza Waziri wa Katiba na Sheria Prof. Palamagamba Kabudi
kuunda timu zitakazoshughulikia biashara ya madini ya Tanzanite na Almasi
pamoja na migodi mingine ya dhahabu haraka iwezekanavyo ili nchi iweze
kunufaika ipasavyo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John
Pombe Magufuli akishuhudia Mwenyekiti Mtendaji wa Kampuni ya Barrick Gold Corp.
Profesa John L. Thornton akiwa na Afisa Uendeshaji wa Barrick Gold
Richardc William huku Waziri wa Sheria na Katiba Profesa Palamagamba Kabudi na
Florens Luoga nao pia wakiweka saini ripoti ya makubaliano baina ya Kamati ya
Serikali na timu ya wataalamu wa Barrick Gold kuhusu bishara ya madini
Ikulu jijini Dar es salaam.
Agizo
hillo Rais Magufuli amelitoa leo jijini Dar es Salaam wakati akipokea taarifa
ya majadiliano kati ya Tanzania na timu ya wawakilishi wa kampuni ya Barrick
Gold inayomiliki migodi ya madini hapa nchini ambayo yamekamilika na
makubaliano kati ya pande hizo kutiwa saini mbele yake.
“Nataka machimbo
yote ya dhahabu mchakato kama huu ufanyike, pia nakuagiza Prof. Kabudi biashara
ya madini ya Tanzanite na Almasi nako ni lazima kufuate utaratibu huu,
asiyetaka aondoke” amesema Rais Magufuli.
asiyetaka aondoke” amesema Rais Magufuli.
Aidha amewataka Watanzania kuunga mkono juhudi hizi
badala ya baadhi yao kuzibeza kwa kuwa zina manufaa kwa taifa na wananchi
wake.
Amezipongeza
timu zote mbili yaani Tanzania na Barrick Gold Corporation kwa kazi kubwa
ziliyofanya kufikia makubaliano hayo na kwa kipekee amempongeza Prof. Thornton
kwa nia yake thabiti ya kukubali kufanyika kwa mazungumzo na kukubali mambo
yaliyofikiwa.
Rais
Magufuli amesema makubaliano hayo yataisaidia nchi kuzalishaji ajira zaidi,
kupata manufaa mbalimbali yanayostahili ikiwemo fedha za kugharamia huduma za kijamii kwa wananchi na yanajenga msingi imara ambao utaiwezesha Tanzania
kunufaika na rasilimali zake za madini.
Timu ya
Barrick Gold Corporation ilikuwa imeongozwa na Mwenyekiti Mtendaji wa kampuni
hiyo Prof. John Thornton wakati timu iliyowakilisha Serikali ya Tanzania
imeongozwa na Waziri wa Katiba na Sheria Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko
Kabudi.
Miongozi
mwa mambo waliyokubaliana ni kutekeleza mwelekeo mpya wa biashara ya madini ambapo
kutakuwa na mgawanyo sawa wa faida (yaani Tanzania kupata asilimia 50 na
Barrick Gold Corporation kupata asilimia 50 ya faida) na kuundwa kwa kampuni ya
ubia wa usimamizi wa migodi ya madini iliyopo Tanzania ambayo itakuwa na makao
makuu yake Mwanza na ofisi ndogo Dar es Salaam nchini Tanzania badala ya nchini Uingereza.
Mengine ni
kufunga ofisi za uhasibu na fedha zilizopo Johannesburg Afrika Kusini na kuhamishia Tanzania na kutekeleza masharti yote ya mabadiliko ya sheria mpya ya
madini na rasilimali za nchi ya mwaka 2017.
Aidha, Barrick
Gold Corporation imekubali kuwepo kwa wawakilishi wa Serikali katika bodi za
migodi yake yote hapa nchini, kazi mbalimbali za kwenye migodi kufanywa na
kampuni za Kitanzania, Migodi kutoa ajira za kudumu kwa wachimbaji, wachimbaji
hao kuishi majumbani kwao badala ya kuishi kwenye makambi ya migodi na mashauri
yote ya kesi mbalimbali kufanywa hapa nchini.
Kampuni ya
Barrick Gold pia imekubali kutoa Dola za Kimarekani Milioni 300 sawa na takribani
Shilingi Bilioni 700 kama malipo ya kuonesha nia njema ya kufidia fedha
zilizotokana na upotevu wa mapato kupitia biashara ya kampuni hiyo.
Akizungumza
baada ya kutia saini makubaliano hayo Prof. Thornton amempongeza Rais Magufuli
kwa msimamo wake unaojenga misingi ya biashara ya kuaminiana na uwazi, ambayo
ni muhimu na ya namna
yake kwa
biashara katika karne hii ya 21.
Prof.Thornton
amesema Barrick Gold Corporation watazingatia makubaliano haya na wanaamini kuwa yamefungua ukurasa muhimu utakaowezesha kufanya biashara kisasa.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimlaki Mwenyekiti Mtendaji wa Kampuni ya Barrick Gold Corp.Profesa John L. Thornton alipokutana nae wakati wa kupokea ripoti ya makubaliano baina ya Kamati ya Serikali na timu ya wataalamu wa Barrick Gold kuhusu bishara ya madini Ikulu jijini Dar es salaam leo
No comments:
Post a Comment