Serikali yatangaza ajira 400 TRA...Soma habari kamili na Matukio360..#share


KATIKA kukabiliana na changamoto ya upungufu wa watumiahi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) serikali inatarajia kuajiri wafanyakazi 400 katika kipindi kifupi kijacho.


Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) (aliyesimama) akizungumza na viongozi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) mkoa wa Shinyanga kuhusu nia ya Serikali katika kuhakikisha kodi ya majengo na mabango inakusanywa kikamilifu kwa manufaa ya wananchi na Taifa, alipofanya ziara ya kikazi katika mkoa huo.

Hayo yamebainishwa jana mjini Shinyanga na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Ashatu Kijaji, wakati akizungumza na viongozi na watumishi wa TRA katika ziara yake ya kikazi ya kukagua utendaji wa Mamlaka hayo mkoani humo, amesema hatua hiyo inatarajia kungeza ufanisi wa kazi na makusanyo ya kodi.

Dk. Kijaji amesema kuwa taratibu zote zimekamilika na wakati wowote nafasi za ajira zitatangazwa na kwamba nafasi hizo zimelenga kuiwezesha TRA kuwafikia watu wengi zaidi na kuongeza wigo wa makusanyo ya kodi.

“Tunatambua  changamoto ya uchache wa watumishi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania TRA ndio maana tumeamua kuajiri wafanyakazi hao 400 ambao ni wengi kuliko kada nyingine ili tuweze kuimarisha utendajikazi wa Mamlaka na hivyo kuongeza makusanyo ya kodi zinazotakiwa kwa shughuli za maendeleo nchini” alisema Dk. Kijaji.

Alisema kuwa pamoja na uhaba wa watumishi, anaamini kuwa lengo la mwaka huu la kukusanya shilingi trilioni 17 ambazo Mamlaka hayo imepangiwa yatafikiwa na ikiwezekana kuzidi kwa kutumia wafanyakazi waliopo.

Dk. Kijaji alitoa rai kwa wafanyakazi wa TRA kuwa waadilifu na kwamba atakayebainika kukiuka maadili yake ya kazi atachukuliwa hatua kali za kinidhamu na kisheria.

Awali Meneja wa TRA mkoa wa Shinyanga Jumbe Samson, 
alieleza kuwa mkoa wake umepangiwa lengo la kukusanya Shilingi bilioni 18 na kwamba wanauhakika wa kufikia lengo hilo kutokana na mikakati mbalimbali waliyojipangia ikiwemo kusimamia ukusanyaji kodi kikamilifu katika sekta ya madini.

Kwa upande wake, Kaimu Kamishna Mkuu wa TRA Beatus Nchota alisema kuwa Mamlaka yake imejiwekea mipango ya kufungua ofisi zake kila wilaya hapa nchini ili kusogeza huduma karibu na wananchi na kuongeza wigo wa ukusanyaji wa mapato ya Serikali ili lengo walilopewa la kukusanya shilingi trilioni 17 liweze kufikiwa.

Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Josephine Matiro, akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa mkoa wa Shinyanga, alisema kuwa Serikali mkoani humo itahakikisha kuwa TRA inatimiza malengo yake ya kukusanya kodi na  kumhakikishia Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Ashatu Kijaji kwamba watasimamia kikamilifu ukusanyaji wa mapato ya Serikali.

Naibu Waziri huyo aliwasisitiza watumishi wa TRA mkoa wa Shinyanga  kuhakikisha wanafanyakazi kwa bidii ili kufikia malengo yaliyowekwa na Serikali ya kukusanya Shilingi trilioni 17.



Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) akiwa katika picha ya pamoja na viongozi na watumishi wengine wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) mkoa wa Shinyanga, alipofanya ziara ya kikazi kukagua namna Mamlaka hayo inavyokusanya kodi.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini-Wizara ya Fedha na Mipango)​

About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search