Kesi ya Mbowe na Wenzake kusikilizwa Aprili 16, 2018...soma habari kamili na matukio360...#share

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu inatarajia kusikiliza kesi
inayowakabili viongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) akiwemo
Mwenyekiti wa chama Freeman Mbowe Aprili 16, 2018.
Hatua hiyo inatokana na uamuzi wa hakimu Wilbard Mashauri baada
ya kukubaliana na mapendekezo ya upande
wa utetezi kufanyika kwa usikilizwaji wa awali.
Awali upande wa mashtaka katika kesi hiyo uliiomba Mahakama hiyo
kuruhusu kesi isikilizwe kwa haraka,
ikiwezekana kuanza kesho.
Wakili huyo wa Serikali, Faraja Nchimbi alisema msingi
wa maombi hayo ni kutokana na upelelezi kukamilika.
Alisesema sababu nyingine ni kwamba washtakiwa wengi katika kesi
hiyo ni wabunge na kwa kuwa kesi hiyo inavuta watu wengi ni vema ikasikilizwa
haraka.
"Kwa hiyo tunaomba kama ikiwezekana kesho mchana tuendelee
na usikilizaji wa awali ili sisi upande wa mashtaka tuweze kuwasilisha kile
tulicho nacho,” amesema Nchimbi.
Hata hivyo, wakili wa upande wa utetezi, Peter Kibatala
alipinga mapendekezo hayo akieleza kuwa ndiyo kiongozi wa jopo la mawakili wa
utetezi, kesho atakuwa na kesi nyingine Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi na
kesho kutwa pia atakuwa na kesi nyingine.
Alisema Aprili watakuwa na semina za mawakili ambazo ni za
lazima kwa kuwa bila kupata alama zinazohitajika kutokana na semina hizo,
leseni yake haiwezi kuhuishwa.
Vilevile, alisema kuanzia Aprili 13 watakuwa na mkutano wa
mawakili wote jijini Arusha na akapendekeza usikilizwaji wa awali
wa kesi hiyo ufanyike Aprili 16.
Hakimu Mashauri ameahirisha kesi hiyo hadi tarehe hiyo,
itakapoitwa kwa ajili ya usikilizwaji wa awali.
Mbali ya Mbowe viongozi wengine walioachiwa kwa dhamana ni
Katibu Mkuu Dk Vicent Mashinji, Manaibu Katibu Wakuu John Mnyika (Bara),
Salum Mwalimu (Zanzibar), Mbunge wa Iringa mjini Mchungaji Peter Msigwa,
Mweka Hazina wa Baraza la Wanawake wa chama hicho Ester Matiku na
mwenyekiti wa baraza hilo, Halima Mdee.
No comments:
Post a Comment