WAZIRI MWIGULU ATOA NENO KUHUSU 'WANAOFURAHIA' MAUAJI YA ASKARI
Viongozi kadhaa wa Jeshi la Polisi nchini wameshangazwa na kitendo cha baadhi ya wananchi wa Mkoa wa Pwani kufurahishwa na tukio la mauaji ya askari nane katika Wilaya ya Kibiti waliokuwa wametoka lindoni.
Askari hao waliokuwa wakimalizia doria yao ili kukamilisha zoezi la kuwalinda wananchi pamoja na mali zao, walishambuliwa na wahalifu na kuuawa katika kijiji cha Jaribu kilichoko wilayani hapo.
Kitendo cha baadhi ya wananchi kufurahia na kushindwa kutoa ushirikiano katika tukio hilo linaonyesha kuwa kuna siri nzito iliyofichika.
Akizungumza wakati wa kutoa salamu za rambirambi katika eneo la Polisi Barracks ambako miili ya askari hao iliagwa rasmi, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mwigulu Lameck Nchemba alisema hali inaonyesha wazi kuwa wananchi wanafurahishwa na tukio hilo na huenda wakawa wanawajua wahusika waliofanya uhaifu huo.
“Kwa kiasi kikubwa wananchi wameonekana kufurahishwa na jambo hili, hili ni kwa kuwa wananwajua wahusika na ndio maana vitendo hivi vinaendelea. kitendo hiki si cha bahati mbaya bali kilipangwa, waliofanya watambue kuwa watashughulikiwa kwa mazingira hayohayo kwa kuwa hawajatoka mbali. Wapo eneo hilohilo, Wananchi tunawaomba mtoe taarifa za watu hao kwa hiari la sivyo tutatumia nguvu kuzipata”alisema Migulu
Mwigulu alisisitiza kuwa wanaofanya mauaji maeneo mbalimbali nchini siyo wageni bali ni wenyeji wanaoishi na kuyatambua maeneo hayo vyema. Vilevile aliwataka viongozi wote wa Jeshi la Polisi kukutana ili kupangiana majukumu ikiwa ni kuashiria kuanza rasmi kazi ya operesheni.
Kwa upande wake Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP) Ernest Mangu, alisema tukio hilo ni la kusikitisha kwa kuwa ni mara ya pili kutokea kwa askari ambao wanakuwa kazini.
Aliongeza kuwa matukio hayo huwa yanafanywa na watu ambao hawataki nchi iwe na amani na kwamba hawatawavumilia watu haowanaoonyesha wamejipanga kuwakatisha tamaa jeshi la Polisi.
“Tutachukua hatua hadi watapatikana waliohusika na kushughulikiwa kwa mujibu wa sheria, tunatambua wananchi wa Mkuranga, Kibiti na Ikwiriri wanawajua wahalifu wanaotumia maeneo hayona wanaishi nao na hawataki kuwataja” alisema IGP Mangu.
Vilevile aliahidi kuwa Jeshi la Polisi litawachukulia hatua wale wote walioandika maneno ya kejeli katika mitandao ya kijamii na kusisitiza kuwa watakamatwa na kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria ili iwe fundisho.
Naye Kamanda wa Polisi mkoa wa Pwani, Onesmo Lyanga, alisema tukio hilo ni la kusikitisha kwa kuwa jikumu walilokuwa wakilitekeleza ni halali na kwamba hiyo inawapa fursa nyingine ya kujipanga zaidi kukabiliana na wahalifu.
“Damu hiyo haiwezi kumwagika bure, tutahakikisha wahusika waliofanya kitendo hicho cha kiharamu wanakamatwa na kushughulikiwa ipasavyo” alisema
Askari waliouawa ni pamoja na Mkaguzi msaidizi, Peter Kigugu, koplo francis, PC Haruna, PC Jackson, PC Zacharia, PC Siwale, PC Maswi na PC Ayoub. askari aliytajwa kuwa na umri mkubwa amezaliwa 1979 na mwenye umri mdogo amezaliwa 1995.
Wahalifu hao walipora bunduki 7 zikiwemo SMG 4.
No comments:
Post a Comment