nEWS: ACT wamshukia Waziri Tizeba,.. wamtaka ang'atuke kwa kushindwa kazi...#share.


CHAMA cha ACT -Wazalendo kimemtaka Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Dk. Charles Tizeba kujiuzulu kwa kushindwa kuwapelekea wakulima wa korosho pembejeo kama alivyoahidi.


Mbali na kumtaka waziri huyo kujiuzulu, pia kimetoa mapendekezo 14, likiwemo la kuitaka Serikali kufanya haraka kutimiza ahadi yake ya kufikisha pembejeo ya bure kwa wakulima wa korosho, kwa kuhakikisha inafikisha kiwango cha pembejeo kinacholingana na mahitaji yaliyoko.

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam, Katibu wa kamati ya Itikadi, Mawasiliano ya Umma na Uenezi wa chama hicho, Ado Shaibu alisema Serikali iliahidi kupeleka tani 5,000 za sulphur lakini imepeleka tani 1,500 tu.

“Matokeo yake wafanyabiashara wanauza sulphur hadi kufikia Sh 80,000 kwa mfuko mmoja badala ya Sh30,000,” alisema.

Kufuatia hali hiyo, chama hicho kimeitaka Serikali kufanya uchambuzi wa kina wa mahitaji halisi ya kila mkulima na kuwa na uhakika wa bejeti yake ndipo itangaze na kutekeleza mfumo wa sulpher  ya bure na isikurupuke tu kwa lengo la kutaka sifa.

Amebainisha kuwa serikali inapaswa kufungamanisha sekta ya korosho na hifadhi ya jamii ili kupitia fao la bei kuweza kuweka uimara wa bei za mazao na pembejeo.

“Fao la bei litalinda ustawi wa wakulima wa korosho na kuwaepusha na hasara iwapo bei ya korosho ya msimu huu itaanguka tofauti na msimu uliopita,” alisema,

Amesema kuwa Mei mwaka huu, kwenye kikao cha mwaka cha wadau wa zao la korosho kilichofanyika mjini Dodoma, Serikali ilitangaza uamuzi wa kugawa pembejeo bure kwa wakulima wote wa zao la korosho.

Amesema uamuzi huo ulitangazwa na Dk  Tizeba mbele ya Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye mkutano huo.

Amesema kutangazwa kwa uamuzi huu kuliibua shangwe kubwa kwa wakulima wa korosho ambao walifurahia kupunguziwa mzigo wa kununua pembejeo.

“Uamuzi huu ulileta matokeo yafuatayo, Mfumo wa Pembejeo ya ruzuku ulifutwa. Kabla ya mfumo wa kugawa pembejeo bure kutangazwa, kulikuwa na mfumo wa pembejeo uliokuwa ukiendeshwa na Vyama vya Msingi vya ushirika (Amcos),”

“Vyama hivi vya msingi vya ushirika vilikuwa vinakusanya fedha kwa wakulima wakati wa mauzo (kiasi cha shilingi 15,000 tu kwa mfuko), kununua pembejeo nje ya nchi na kugawa kwa wakulima,” alisema Shaibu.

Aidha amesema kabla ya kutangazwa kwa uamuzi huu, vyama vya msingi vya ushirika (Amcos) vilikuwa vimeshakusanya fedha kwa wakulima na vinajipanga kununua Salfa nje ya nchi. Kwa uamuzi huo wa serikali, vyama vya ushirika viliamriwa kuwarudishia wakulima fedha zilizokusanywa kwa sababu ‘Pembejeo ya bure’ ingeletwa.

Na Abraham Ntambara

About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search