eXCLUSIVE: Lipumba, Maalim waendelea Kushikana 'Uchawi'....#share
MWENYEKITI wa Chama cha Wananchi (CUF) anayetambuliwa na
Msajili wa Vyama vya Siasa, Profesa Ibrahim Lipumba amesema Katibu Mkuu wa
chama hicho, Maalim Seif Sharif Hamad ameshindwa kutekeleza majukumu yake kama
kiongozi, huku akimtaka kurejea ofisini kuendelea na majukumu yake.
Wakati Lipumba akisema hayo na kudai kuwa majukumu ya
Maalim Seif yanakaimiwa na Naibu Katibu
Mkuu, Magdalena Sakaya, Naibu Katibu Mkuu wa Chama hicho-Zanzibar, Nassor Ahmed
Mazrui amesema Maalim Seif hawezi kufanya kazi na Lipumba na kubainisha kuwa
sasa wanapambana na Dola si msomi huyo.
Leo wakati akihojiwa na kituo kimoja cha televisheni,
Profesa Lipumba alisema bado anamtambua Maalim Seif kama Katibu Mkuu wa chama
hicho licha ya utoro wake kazini.
Katika mahojiano yake ya jana, Profesa Lipumba alisema, "Sijamwona
Katibu Mkuu tangu Septemba 23 mwaka jana, namkaribisha aje ofisini Buguruni
apokee maelekezo kutoka kwa mwenyekiti.”
Mwenyekiti huyo amesisitiza kwamba yeye ni mwenyekiti
halali wa CUF kwa mujibu wa ibara ya 117 ya chama hicho ambayo inaeleza
taratibu za kiongozi kujiuzulu.
"Ibara ya 117 inatoa mamlaka kwa mkutano mkuu
kujadili barua ya kiongozi kisha kuridhia kujiuzulu kwake au laa. Sasa mimi
niliandika barua ya kutengua kujiuzulu kabla mkutano mkuu wa chama haujakaa
kuijadili barua yangu ya kujiuzulu," alisema.
Profesa Lipumba amesema chama chake kilifuata taratibu
zote za kuwavua uanachama wabunge wanane ambao walibainika kukihujumu chama
hicho.
Amesisitiza kuwa yuko tayari kumaliza mgogoro unaondelea
kwa vikao vya ndani ya chama, hata hivyo anasikitika kwamba hasimu wake hayuko
tayari kwa meza ya mazungumzo.
Akijibu hoja za Profesa Lipumba, Mazrui amesema, “Lipumba
hatuwezi kumsikiliza kwa sababu tunajua
anayoyafanya ametumwa na mwenye nchi. Hata aseme nini hatumsikilizi. Hivi ni
vita kati ya CUF na Dola, si CUF na Lipumba.”
Amesema vita hivyo vinalenga kuua upinzani na tayari
wameshajua wanapambana na nini, kubainisha kuwa Msajili wa Vyama vya Siasa na
Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) pamoja na Bunge si wajinga bali wanashinikizwa
na Ikulu.
“Lipumba apige kelele hadi apasuke na uzuri ni kwamba
tumeshamfukuza na si mwenyekiti wetu tena. Kwa sasa tunaangalia jinsi gani ya
kufanya kuhakikisha hali inatulia na demokrasia inarejea,” alisema Mazrui.
“Yeye aseme mpaka apasuke sisi hatumsikilizi.
Maalim Seif hawezi kwenda kufanya kazi
na Lipumba na huyo anayejiita mwenyekiti pia hawezi kufanya kazi na CUF
inayotambulika.”
Na Mwandishi wetu.
No comments:
Post a Comment