nEWS: ACT- Wazalendo waja na Ujenzi wa Taifa Huru la Kidemokrasia kwa Maendeleo Endelevu...#share

CHAMA cha ACT- Wazalendo kinatarajia kufanya Mkutano Mkuu wa Kidemokrasia wa Tatu wenye dhima ya “Ujenzi wa Taifa Huru la Kidemokrasia kwa Maendeleo Endelevu”

Hayo yalibainishwa jana jijini Dar es Salaam na  Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho Bara, Msafiri Mtemelwa akizungumza na waandishi wa habari, alisema utafanyika jijini Mwanza Agosti 26 mwaka huu.

“Maada mbalimbali kwenye maeneo ya Uhuru, Demokrasia na Maendeleo zitawasilishwa,” alisema Mtemelwa.

Aidha alisema kwa mujibu wa Ibara ya 29(7) ya Katiba ya ACT toleo la Mwaka 2015, Mkutano Mkuu wa Kidemokrasia ni jukwaa la mjadala kuhusu masuala mbalimbali ya kitaifa na kimataifa kwenye nyanja za siasa, uchumi na utamaduni.

Alisema mkutano huo utawaleta pamoja viongozi wa ngazi mbalimbali na wanachama wa chama hicho  kutoka pande mbalimbali za nchi, wanasiasa wa vyama mbalimbali wa ndani na nje ya nchi, wanaharakati mbalimbali, wadau wa maendeleo, watetezi wa haki za binadamu na wananchi wa kawaida wasio wanachama wa vyama vya siasa.

Matemelwa alibainisha kwamba  mbali na wageni wa ndani, wametuma mialiko kwenye vyama na taasisi mbalimbali za nje ikiwemo vyama vya Die Linke (Ujerumani), The Altenative (Denmark), PIC Senegal (Senegal), Cyriza (Ugiriki), Labour (Uingereza), na Red Green Alliance (Denmark).
Aliwakaribisha Watanzania wote kushiriki kwenye mkutano huo mkubwa wa kihistoria.
Kwa upande mwingine Mtemelwa alisema mkutano huo pia  utakuwa jukwaa mahsusi la kupaza sauti kuhusu kero za makundi mbalimbali kwenye jamii na jinsi ya kuzitatua. Alitaja kuwa ni pamoja na sekta ya kilimo cha korosho na suala la ajira, rasmi na zisizo rasmi.
Alisema kwenye suala la ajira watazungumzia suala la Sekta ya Walinzi Binafsi ambayo ilianza kuchanua nchini miaka ya themanini kama sehemu ya mageuzi ya kiuchumi na kisiasa.
Alieleza hadi sasa, Tanzania inakadiriwa kuwa na walinzi wa sekta binafsi zaidi ya milioni mbili. Kundi hilo limeachwa kwenye madhila makubwa bila kuwa na sauti ya utetezi.

Alitaja baadhi ya changamoto za Sekta ya Walinzi Binafsi ni Tanzania kutokuwa na sheria mahsusi ya sekta hii kama ilivyo kwa nchi nyingine kama nchi ya Afrika ya Kusini, sekta hii inatambulika kikatiba (Ibara ya 199(3) ya Katiba ya Afrika ya Kusini) na inayo sheria mahsusi inayoisimamia (The Private Security Industry Regulations Act, 2001).

Aidha alisema nyingine ni kampuni nyingi kulipa mshahara duni kwa walinzi ukilinganisha na kazi ngumu wanayofanya. Alibainisha mishahara hiyo kuwa ni kati ya sh. 70,000 hadi sh. 150,000.

Aidha alisema uchambuzi mpana utafanyika kwenye mkutano huo wa Kidemokrasia na watahudhuria wadau mbalimbali wa sekta ya ulinzi binafsi hasa walinzi wenyewe.

About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search