KAMATI ya Uchunguzi upotevu wa Madini ya Almasi Yawakaanga wajumbe wa bodi na wote waliohusika kusimamia Mgodi...Pia wamo Mawaziri Wamagufuli....#share

KAMATI ya Bunge iliyoundwa kuchunguza upotevu wa madini ya Almasi, imependekeza wajumbe wote wa bodi na watu waliohusika na kusimamia mgodi wa madini hayo, wahojiwe na ikibainika wamehusika wachukuliwe hatua.

Akisoma ripoti ya kamati hiyo ambayo ilikabidhiwa kwa Spika wa Bunge, Job Ndugai ambaye naye alimkabidhi Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, Mwenyekiti wa kamati hiyo, Mussa Azan Zungu amesema wamebaini madudu mengi.

Madudu hayo ni pamoja na upotevu wa kodi, kutosimamiwa vyema kwa uchimbaji wa madini hayo, tofauti kubwa kati ya takwimu zinazotolewa na taasisi za Serikali juu ya kiasi kilichopatikana na kuuzwa cha madini hayo na udanganyifu kuhusu hali na gharama za mitambo.
“Kamati inapendekeza Serikali iwahoji wajumbe wa bodi ya migodi hii na wote wanaohusika na ikibainika kuwa walihusika katika mapungufu waliyoyaona wachukuliwe hatua,” alisema Zungu.
Watendaji hao wa Serikali pamoja na wajumbe wa bodi za madini ni, aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini katika Serikali za Awamu za Nne na Tano, Profesa Sospeter Muhongo.
Wengine ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Tamisemi), George Simbachawene, aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini katika Serikali ya Awamu ya Nne, William Ngeleja, na Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Edwin Ngonyani pamoja na Waziri wa Nishati na Madini wa Serikali ya Awamu ya Tatu, Maokola Majogo.
Watendaji wengine ni aliyekuwa Katibu Muu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakim Maswi, Profesa Abdulkarim Hamis Mruma na Profesa Isaya Jairo.
Akizungumza kuhusu takwimu hizo, Zungu alisema takwimu zilizokuwepo kwa Wakala wa Madini Tanzania (TIMA) zinaonesha kuwa kuanzia mwaka 2007 hadi 2017, kiasi cha karati milioni 1.5 zilizalishwa na kuuzwa kwa dola za Marekani milioni 374.5 sawa na sh bilioni 823.9.
Kwa upande wa Wizara ya Nishati na Madini, takwimu zilizokuwepo zilionesha kuwa ni karati milioni 1.4 ndizo zilizozaliswa na kuuzwa kwa dola za Marekani milioni 362 ambazo ni sawa na sh bilioni 796.4 huku tofauti ikiwa ni sh milioni 27.5.

Na Mwandishi Wetu

About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search