Manispaa ya Ilala Imesema leo kuwa Vitendo vya Ukatili kwa Watoto Vimepungua Kutoka kesi....#share
HALMASHAURI ya Manispaa ya Ilala imesema vitendo vya ukatili wanavyofanyiwa watoto chini ya miaka 18 vimepungua kutoka kesi 199 zilizoripotiwa kwenye vituo vya polisi kwa mwaka 2016 hadi kesi 109 ziliropitiwa kwenye vituo hivyo kwa mwaka 2017.
Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam Ofisa Mkuu wa Idara ya Jamii na Ustawi wa Jamii na Vijana wa Manispa hiyo Francisca Makole akitoa taarifa ya mwaka ya maendeleo ya ukatili katika halmashauri ya wilaya ya Ilala, amesema vitendo hivyo vimepungua kutokana na elimu wanayotoa kwa jamii.
Amesema kutokana na elimu hiyo kumekuwa na ushirikiano unaotolewa na jamii hususani katika kuripoti matukikio hayo ya ukatili kwa watoto kwenye mamlaka husika. Alibainisha pia ukatili wa kingono umepungua kutoka asilimia 32 kwa mwaka jana hadi kufikia asilimia 19 kwa mwaka huu.
“Sahivi watu wamekuwa mstari wa mbele kutoa taarifa pindi mtu anapofanyiwa ukatili wowote katika jamii,hususani kutoa taarifa kwenye kituo cha mkono kwa mkono ambacho kinatumika kutoa huduma ya kupinga ukatili wa kijinsia,hii imechangia kupungua kwa vitendo vya ukatili’’ amesema Makole.
Makale amesema kwa sasa wamekuwa wakishirikiana na watu mbali mbali ambao wanajitolea kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia ili kuweza kutokomeza vitendo vya ukatili wa kijinsia ndani ya manispaa hiyo.
Mratibu wa kituo cha kupokea malalamiko ya watu wanaofanyiwa vitendo vya kijinsia cha One stop center , Sufian Mrisho amesema licha ya jamii kutoa ushirikiano kwa kutoa taarifa mapema pindi wanavyofanyiwa vitendo hivyo lakini bado jamii imekuwa ikipoteza ushahidi wa kuwati hatiani wanaofanya vitendo vya ukatili.
‘’Moja ya Changomoto tunayokumbana nayo ni watu wanaofanyiwa vitendo vya ukatili ni kupoteza ushahidi ikiwemo kwenda kuoga mara baada ya kufanyiwa vitendo vya ubakaji na matokeo yake kupeza ushahidi na hili linachangia hata kesi hizi kuwa ngumu mahakamani” amesema Sufiani.
Katika hatua nyingine Manispaa ya Ilala imesema watu wanaohusika kufanya vitendo vya omba omba sio wakazi wa minispaa hiyo kama ambavyo inasemwa na watu.
Makale ameeleza kwa uchunguzi waliofanya wamebaini asilimia 90 ya watu wanaofanya vitendo hivyo wanatoka kwenye Wilaya ya Bahi Mkoani Dodoma ambapo wamekuwa wakiletwa na watu huku wakitumikishwa kufanya vitendo hivyo.
Akizungumzia hatua mbali mbali zilichokuliwa na manispaa hiyo kutokomeza vitendo vya Omba omba , Ofisa Ustawi wa jamii wa Manispaa hiyo, Joyce Maketa amesema kwa sasa wako mbioni kutunga sheria ambayo itaweza kumaliza vitendo hivyo.
“Kwa sasa tupo katika hatua ya mwisho kutunga sheria ambayo itambana anayetoa hela kwa omba omba na hata yule omba omba atayechukua ambapo wataweza kupigwa faini hili ni itakuwa lengo zuri la kutokomeza vitendo hivi” amesema Maketa.
Amesema wamekuwa wakiwakamata watu wanaofanya vitendo vya Omba omba na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria huku wengi wao wamekuwa wakipewa hukumu mbali mbali kama faini na vifungo vya nje.
Maketa ametoa rai kwa jamii kutokubali kuwaruhusu watoto au kuwavumilia watu wanaofanya vitendo hivyo kwa kusema vitendo hivo havufai kwenye jamii.
Na Abraham Ntambara






No comments:
Post a Comment