Bilioni 702 kujenga barabara mikoani....soma habari kamili na matukio360..#share

Na Abraham Ntambara

SERIKALI imesaini mikataba minne na kampuni nne za ujenzi wa barabara yenye thamani ya zaidi ya  bilioni 702 kwa ujenzi wa kilomita 402.


Tukio hilo kusaini mkataba hiyo limeshughudiwa na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, Mwakilishi Makazi wa Benki ya Mandeleo Afrika (ADB), Hellen Minja, wabunge ambao barabara zitajengwa, wawakilishi wa Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) na wakandarasi walioshinda zabuni.

Akizungumzia utiaji saini huo Waziri Mbarawa amesema fedha hizo zitatumika katika ujenzi wa barabara kutoka Tabora, Usesula hadi Mpanda Katavi kilomita 335 na kilomita 67 kutoka Mbinga hadi Mbamba Bay mkoani Ruvuma.

Mbarawa amesema ujenzi wa barabara hizo ni utekelezaji wa ilani ya CCM na ahadi za rais John Magufuli wakati wa kampeni.

Amesema fedha hizo zimetolewa na ADB ikiwa ni baada ya serikali kuomba msaada mwaka 2015 ili kuweza kufungua fursa zilizopo katika maeneo husika kwa miradi.

Waziri ametumia nafasi hiyo kuwataka wakandarasi walioshinda zabuni kujenga barabara zenye ubora na viwango kwa kuzingatia muda wa ujenzi.

Mbarawa amesema nia ya serikali ni kuona ujenzi wa barabara hiyo unakamilika kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2020.

"Naomba Tanroads msimamie ujenzi wa barabara yenye ubora kwani wakandarasi wengi ni wajanja na ikitokea mtu ameharibu asipewe nafasi kabisa ya ujenzi wa barabara hapa nchini," amesema.

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa Tanroads, Mhandisi Patrick Mfugale amesema wakandarasi waliopewa kazi wametokana na uchambuzi mkubwa uliofanyika kati ya wakandarasi 129 waliojitokeza mwaka 2016.

Amesema ili kurahisisha ujenzi wa barabara hizo wamegawa kwa wakandarasi wanne ambapo barabara ya Usesula hadi Komanga kilomita 108 itajengwa na Kampuni ya Jiangxi Geo-Engineering Group Corporation Limited ya China kwa gharama ya zaidi ya  Sh.Bilioni 158 na itajengwa kwa miezi 36.

"Komanga hadi Kasinde kilomita 108 itajengwa na Mkandarasi Kampuni ya China Wu Yi Co. Limited kwa zaidi ya sh.billioni 140 na Kasinde hadi Mpanda kilomita 105 Mkandarasi Kampuni ya China Railway Seventh Group Co.Ltd kwa sh. Bilioni 133," amesema.

Mfugale amesema barabara ya Mbinga hadi Mbamba Bay kilomita 67  inajengwa na Mkandarasi China Henan International Corporation Group Co.Ltd (Chico) kwa sh. Bilioni 129.

Amesema Tanroads imejipanga kusimamia ujenzi huo kwa kufuata viwango vinavyohitajika vya ujenzi wa barabara nchini.

Mwakilishi Mkazi wa ADB, Minja alisema ofisi yake itaendelea kutoa mchango kwa serikali katika ujenzi wa miundombinu mbalimbali nchini pale watakapo hitajika.

Minja amesema matarajio ya ADB nikuona Tanzania inapata maendeleo kwa haraka na njia rahisi ni kupitia miundombinu.

Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Mhandisi Azack Kamwele ambaye barabara ya Tabora hadi Mpanda inapita jimboni kwake alisema ujenzi huo utafungua fursa mbalimbali za kiuchumi na kijamii.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Nyasa, Mhandisi Stella Manyanya ambaye pia ni Naibu Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji amesema barabara hiyo itakuwa kiungo muhimu kati ya Tanzania, Msumbiji na Malawi.

Amesema Nyasa ina vivutio vingi vya utalii hivyo ujio wa barabara hizo utakuwa njia rahisi ya kuwafikisha watalii eneo hilo.


About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search