Mkuu wa wilaya awapa watendaji wiki moja...soma habari kamili na matukio360..#share


Na mwandishi wetu, Chunya
SERIKALI wilayani Chunya mkoani Mbeya imetoa wiki moja kwa watendaji wa ngazi za kata na vijiji kuhakikisha wanaondoa mifugo iliyoingizwa kwenye maeneo ya hifadhi na vyanzo vya maji.


Mkuu wa wilaya  ya Chunya, Rehema  Madusa 

Agizo hilo limetolewa na mkuu wa wilaya  hiyo, Rehema  Madusa katika mkutano wake na viongozi wa vijiji na kata   uliofanyika kwenye kijiji cha Itumba  na kwamba mifugo  itakayokamatwa  ipigwe mnada kwa mujibu wa sheria za nchi.

"Ninashangazwa mifugo inazidi kuingizwa kila kukicha  na wafugaji kuvamia maeneo ya hifadhi  kwa kuweka  makazi na maeneo ya malisho, sasa watendaji ni jukumu letu kuhakikisha muda uliopangwa hakuna mfugo utakaoonekana katika hifadhi," amesema.

Madusa amesema  mwaka  2016/17 jumla ya Ng'ombe 260,000 zimehakikiwa na kutengewa maeneo ya malisho lakini bado mifugo imezidi kuingizwa kiholela.

"Migufo ni changamoto kubwa ambayo inachangiwa na baadhi ya viongozi wa vijiji kuwabeba wafugaji sasa ni lazima mifugo yote kuondolewa haraka na  watakaoshindwa kutekeleza agizo hilo hatua zitachukuliwa," amesema mkuu huyo wa wilaya.

Diwani wa kata ya Chalangwa, Petro Nelson amesema   uondoaji mifugo unahitaji muda kwa kuwa  mifugo mingi  haijahakikiwa  na hakuna maeneo  yaliyotengwa kwa matumizi bora ya ardhi na malisho ya mifugo.

"Agizo hili tutatekeleza lakini linahitaji muda kwani wafugaji ni wakorofi sana na kuwaondoa kwa ghafla  tutasababisha vurugu kubwa zitakazochangia uvunjifu wa amani,"amesema diwani huyo.

Amekiri  kuwa mifugo inaingizwa  kiholela katika maeneo ya hifadhi, misitu na vyanzo vya maji  lakini ameiomba serikali kutoa muda ili elimu itolewe kwa wafugaji kuhusu madhara na faida.

Hata hivyo mfugaji kutoka  kijiji cha Itumbi, Mabula Shija amesema  wapo tayari kuondoa mifugo katika maeneo ya hifadhi na kuomba Serikali kuona namna ya kuwatengea maeneo ya matumizi bora ya ardhi kwa ajili ya shughuli za malisho ya mifugo.




About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search