Ukatili waendelea kusumbua nchini....soma habari kamili na matukio360..#share

Na Abraham Ntambara, Dar es salaam

KIWANGO cha ukatili wa kijinsia nchini na duniani bado ni kikubwa na kwa mujibu wa taarifa ya afya ya uzazi na mtoto na viashiria vya malaria Tanzania ya mwaka 2015/2016 inaonesha kuwa wanawake 4 kati ya 10 wamewahi kukumbana na ukatili wa kimwili tangu wakiwa na umri wa miaka 15.
Kaimu mkurugenzi mtendaji wa TGNP Mtandao Grace Kisetu akizungumza  na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.

Takwimu hizo zimeelezwa leo jijini Dar es Salaam na mkuu wa wilaya ya Ubungo Kisari Makoro akizungumza katika maadhimisho ya kampeni ya siku 16 za kupinga ukatili wa jinsia iliyoandaliwa na Mtandao wa Jinsia nchini  (TGNP Mtandao).

“Asilimia 42 ya wanawake waliowahi kulewa wamekutana na ukatili wa wenza wao ama wa kimwili au ukatili unaohusisha ngono. Hivyo basi nawaomba watanzania wenzangu katika maeneo yenu pazeni sauti na kufanya kwa vitendo kupinga masuala ya ukatili wa kijinsia unaowakumba sana wanawake na watoto,” amesema.

Amesema kuwa athari za ukatili wa kijinsia ni kubwa katika nyanja za kisiasa, kijamii na kiuchumi kwa mtu mmoja mmoja na taifa. Hivyo ametaka kampeni hiyo ilenge kuinua uelewa wa jamii na wadau mbalimbali kuhusu madharaya ukatili dhidi ya wanawake na watoto.

Mkuu huyo wa wilaya pia amewasisitiza maofisa maendeleo ya jamii na maofisa ustawi wa jamii wa wilaya na kata zote kuweka mipango thabiti ya kuonesha kwamba wanashirikiana na wananchi, polisi kukomesha vitendo hivyo.

Ameongeza kuwa serikali inatekeleza mpango kazi wa kutokomeza ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake na watoto (2017/18-22) na kurekebisha sheria mbalimbali ambazo zinakataza kufanya vitendo vya ukatili wa kijinsia.

Kwa upande wake kaimu mkurugenzi mtendaji wa TGNP Mtandao Grace Kisetu akizungumza kwa niaba ya mkurugenzi mtendaji, amesema lengo kubwa la maadhimisho ya kapmeni hiyo kwa mwaka huu ni kupinga ukatili dhidi ya watoto kwa kuboresha mazingira yatakayomwezesha mtoto wa kike kupata elimu sawa na mtoto wa kiume.

Amesema tafiti zinaonesha kuwa ukatili wa kijinsia umekuwa ni sehemu ya maisha ya wanawake wengi na watoto kwani mmoja kati ya watoto wa kike watatu na mmoja kati ya watoto wa kiume saba amekumbana na baadhi ya matukio ya ukatili wa kingono kabla kabla ya kutimiza miaka 18.

“Asilimia 72 ya watoto wa kike wamekabiliwa na ukatili wa kimwili na kihisia wakati kwa watoto wa kiume ni asilimia 71,” amesema.

Ameongeza kuwa kumekuwa na mila na desturi zinazowaumiza watoto na wanawake nchini na ni kutokana na takwimu kuonesha wanawake wanaolewa wadogo takribani miaka mitano mapema zaidi ya wanaume, zaidi ya asilimia 70 ya wanawake katika baadhi ya jamii wamekeketwa na takribani wanawake na watoto wa kike milioni 7.9 nchini wamekeketwa.

Amesema katika maadhimisho hayo TGNP Mtandao imelenga kuhamasisha uboreshaji wa miundo mbinu na vifaa ili kuimarisha usalama wa watoto wa kike mashuleni.


About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search