Daraja Ruhuhu kukamilika mwezi Juni...soma habari kamili na matukio 360...#share

Na Mwandishi Wetu, Ruvuma

NAIBU Waziri wa Ujenzi, Elias Kwandikwa, amemtaka mkandarasi anayejenga daraja la Ruhuhu wilayani Nyasa, mkoani Ruvuma kuendelea kufanya kazi kwa bidii ili kuhakikisha  anamaliza daraja hilo kwa wakati na kwa ubora unaotakiwa na kwamba ifikapo mwezi Juni,2018 akabidhi.
Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoa wa Ruvuma, Mhandisi Lazeck Alinanuswe (katikati), akitoa taarifa ya mradi wa ujenzi wa Daraja la Ruhuhu lililopo wilayani Nyasa, mkoani humo kwa Naibu Waziri wa Ujenzi, Elias Kwandikwa, wakati alipokagua  daraja hilo kuona maendeleo ya ujenzi wake.

Agizo hilo amelitoa leo Wilayani Nyasa, mkoani Ruvuma alipokuwa akikagua ujenzi wa daraja hilo  ambapo ameusisitiza Uongozi wa Wakala wa Barabara (TANROADS), Makao makuu kuhakikisha kuwa utaratibu wa zoezi zima la ununuzi wa vyuma vitakavyowekwa juu ya daraja hilo linaenda sambamba na makadirio ya muda wa mradi ili kupelekea kazi hiyo kukamilika kwa muda uliopangwa.

"Nafikiri sasa jipangeni vizuri ili masika yakiiisha mhakikishe mnafanya kazi kwa bidii ya hali ya juu, nataka kufikia mwezi Juni daraja liwe limekamilika, pia TANROADS Makao makuu hakikisheni mchakato wa manunuzi ya vyuma vya daraja mnauanza mapema ili kuweza kukamilika mapema, msisubiri hadi daraja hili kukamilika", amesema Naibu Waziri Kwandikwa.

Ameongeza kuwa daraja hilo likikamilika litakuwa ni kiungo kwa watu wa Nyasa mkoani Ruvuma na Ludewa mkoani Njombe kwani wamekuwa wakilisubiri daraja hilo kwa ajili ya kujiendeleza katika shughuli mbalimbali za kiuchumi.

Aidha, amemwagiza Meneja wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), mkoani humo, Mhandisi Elisha Mgira, kuhakikisha anarekebisha kasoro zilizopo kwenye kivuko cha Ruhuhu ili kuweza kufanya kazi katika kipindi hiki ambacho wananchi wanasubiri ujenzi wa daraja kukamilika.

Kwa upande wake, Mhandisi Mkazi wa daraja hilo, Mhandisi Napegwa Kiseko, amesema kuwa Ujenzi wa mradi huo umefika asilimia 50 ambapo kazi zinazofanyika sasa ni kujaza matabaka ya barabara zinazoingia darajani hapo ili kunyanyua tuta la barabara.

Amefafanua kuwa kazi hiyo inaendelea pande zote mbili yaani mkoa wa Ruvuma na Njombe ingawa kwa kipindi hiki cha  mvua kazi hiyo imekuwa na vikwazo vingi.

"Ujenzi wa misingi ya daraja kwa upande wa mkoa wa Ruvuma upo kwenye hatua za mwisho na kwa upande wa Njombe ujenzi wa misingi ulianza mwishoni mwa mwezi Disemba na unaendelea", amesisitiza Mhandisi Kiseko.


Mradi wa ujenzi wa daraja la mto Ruhuhu ambao upo mpakani mwa mkoa wa Ruvuma na Njombe unatarajiwa kugharimu takribani kiasi cha shilingi Bilioni 6 ambazo ni fedha za Serikali kwa asilimia mia moja na unatarajiwa kukamilka mwezi Juni mwaka huu.

About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search