Hivi ndivyo msongamano wa magari Dodoma utakavyopunguzwa....soma habari kamili na matukio360...#share

Na Mwandishi wetu, Dodoma

SERIKALI imesema kuwa ujenzi wa barabara ya Mbande- Kongwa (Km 11.7) na Chimwaga - Ihumwa (Km 10) utasaidia kupunguza msongamano wa magari yanayoingia Dodoma mjini.
Meneja wa  Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoa wa Dodoma, Mhandisi Leonard Chimagu, akimuonesha Naibu Waziri wa Ujenzi, Elias Kwandikwa, sehemu ya ujenzi wa barabara  ya mchepuo kutoka  Chimwaga-Ihumwa yenye urefu wa KM 10 inayojengwa kwa kiwango cha lami  kwa ajili ya kupunguza msongamano  wa magari yanayoingia mkoani humo.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Ujenzi, Elias Kwandikwa, alipokuwa akikagua barabara hizo na kuridhishwa na kasi ya ujenzi wake ambapo amesisitiza kwa wakandarasi wanaojenga barabara hizo kuhakikisha wanamaliza kazi hizo kwa muda uliopangwa na kwa viwango vilivyo kwenye mkataba.

"Tutaendelea kujenga na kuboresha barabara hizi za mchepuo lengo ni kupunguza msongamano katikati ya mji kwani Dodoma sasa inakua kutokana na uwepo wa watumishi wengi wa Serikali na ongezeko la magari, kwa hiyo sisi kama Serikali hatuna budi kuangalia namna ya kuboresha miundombinu yetu ili ikidhi haja ya ongezeko hili", amesema Kwandikwa.

Amefafanua kuwa barabara hizo zikikamilika zitakuwa ni njia mbadala kwa watumiaji kwa kuwa si lazima kwa magari yote kupita mjini na badala yake yatatumia njia nyingine za mchepuo kuendelea na safari zake.

Katika hatua nyingine,  Naibu Waziri Kwandikwa amekagua athari za mvua katika barabara za mji wa Dodoma na kuwataka wananchi  na madereva kuchukua tahadhari ili kuepusha hatari zinazoweza kuwakabili  wakati wakivuka ama kupitisha magari yao  katika kipindi hiki ambacho baadhi ya sehemu za barabara zinajaa maji kutokana na mvua nyingi zinazoendelea kunyesha. 

Amewaomba viongozi mbalimbali wa Serikali  kushirikiana katika kutoa ushauri kwa wananchi kuhusu utafutaji wa maeneo yanayowafaa kuishi ili kunusuru maisha yao na mafuriko ambayo yanaweza kuwakabili kutokana na kuchagua maeneo yasiyo sahihi kwa makazi ya binadamu.

Kwa upande wake, Meneja wa  Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoa wa Dodoma, Mhandisi Leonard Chimagu, amefafanua kuwa  barabara ya Mbande- Kongwa yenye urefu wa  KM 11.7, kwa sasa imejengwa kilometa Tano ikiwa ni awamu ya kwanza na kufikia mwezi ujao watajenga tena kilometa nyingine Tano.

Naye, Msimamizi wa ujenzi wa barabara ya Chimwaga - Ihumwa yenye urefu wa KM 10 kwa kiwango cha lami, Mhandisi Nicholaus Mzeru,  amesema mradi ulianza mwaka 2013, ambapo kwa sasa umefika asilimia 92.4 na kilometa 8 tayari zimeshajengwa.

Ujenzi wa Barabara ya Chimwaga- Ihumwa (Km 10), inajengwa na mkandarasi Nyanza Road Works kwa gharama ya takriban shilingi bilioni 15 ambapo ujenzi wake unaendelea na unategemewa kukamilika mwezi Aprili mwaka huu.


About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search