Wabunge CUF wamwandikia barua rais wa FIFA....soma habari kamili na matukio360...#share

Na Abraham Ntambara, Dar es Salaam

WABUNGE wa Chama cha Wananchi CUF wamemuandikia barua ya wazi Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Duniani (FIFA) Gianni Infantino, kumwelezea kilio cha Wazanzibar kuhitaji haki yao ya Zanzibar kuwa mwanachama FIFA.
Mnadhimu wa Kambi ya CUF Bungeni Ally Saleh akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.

Pia wamesema watafungua shauri mahakamani ili kutafuta uhalali wa kikatiba wa chombo cha Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini (TFF) kufanya kazi ya muungano na iizuie TFF kufanya kazi yoyote mpaka uamuzi utakapotolewa.

Hayo yameelezwa na Mnadhimu wa Kambi ya CUF Bungeni ambaye pia ni Mbunge wa Malindi, Zanzibar Ally Saleh alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam kwa lengo la kuufahamisha umma juu  ya barua waliyoandika kwenda kwa rais huyo wa FIFA.

“Sisi wabunge wa wananchi tunathamini juhudi zinazochukuliwa na kuipigania Zanzibar, lakini kuna msemo wa Kiswahili unaeleza ukibebwa ujikaze na pia mwengine unaosema mshike mshike na mwenyewe uko nyuma,”

“Kwa sababu hiyo basi pamoja na mazungumzo ambayo yatafanywa kuendelea kuishawishi FIFA ielewe hali ya Zanzibar basi na sisi tumeona pia tupaze sauti zetu hasa kwa sababu viongozi wa FIFA wapo nchini lakini zaidi kwa sababu rais wa taasisi hiyo yupo nchini, hivyo tumemwandikia barua ya wazi,” amesema na kuongeza Saleh.

Saleh amesema katika barua hiyo wamemweleza mambo siti, mambo hayo ni TFF haiwakilishi maslahi ya Zanzibar, mamlaka ya TFF haijawahi wala hayafiki Zanzibar, muundo wa TFF ni kuwa na vyama vya mikoa, wakati ZFA ina mikoa yake.

Mengine ni TFF haijawahi kuwa na sera ya maendeleo inayohusisha Zanzibar, TFF inasimamia Kilimanjaro Stars na kuifanya timu ya Taifa Stars na mwisho hakuna kikao chochote cha kikatiba baina ya TFF na ZFA.

Amesema pamoja na kwenda mahakamani kutafuta uhalali wa TFF kufanya kazi ya muungano, ametaja mambo mengine watakayotaka kupatiwa ufafanuzi na mahakama ili waweze kufanikiwa kupata haki yao ya uanachama wa FIFA.

Ametaja kuwa ni kuitaka mahakama iwape muongozo juu ya kwa nini pasiwepo chama cha soka cha Tanzania Bara na kutafuta tafsiri ya waziri wa michezo wa Tanzania Bara kutumika kama ni waziri wa muungano ndani na nje ya nchi.
Pamoja na hayo amebeinisha kuwa watatoa hoja binafsi bungeni kuhusu mustakabali ya michezo chini ya utaratibu tata uliopo hivi sasa.

“Tunaamini bila kufanya hatua hiyo hapatakuwa na suluhu kwa sababu hali hii imeendelea kwa muda mrefu na tumekuwa tukijificha kama mbuni kufanya kana kwamba sababu ya Zanzibar kukosa uanachama wa FIFA haitokani na muungano na muundo wake,” ameeleza Saleh.



About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search