Wanawake ACT-Wazalendo watoa neno kwa serikali...soma habari kamili na matukio360...#share


Na Abraham Ntambara, Dar es Salaam

CHAMA cha ACT-Wazalendo kupitia Ngome ya Wanawake kimeitaka serikali kuacha ukandamizaji wa Demokrasia na haki za binadamu.

Msimamo huo umetolewa leo jijini Dar es Salaam na Mwenyekiti Ngome ya Wanawake Taifa wa chama hicho, Chiku Abwao alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu hali na mwenendo  wa siasa na haki za binadamu nchini.

“Tunaitaka serikali ya Jamhuri ya muungano wa Tanzania chini ya Rais Magufuli iache ukandamizaji wa demokrasia na haki za binadamu. Ni muhimu nchi iendeshwe kwa kufuata misingi ya haki na utu,” amesema Abwao.

Amesema nchi inayominya haki haki dhidi ya wananchi wake huzaa taharuki, hofu na hali ya unyonge hivyo ni rahisi kutumbukia katika machafuko kwa kuwa wananchi watachoka kukandamizwa, kubuluzwa, kunyanyaswa na kuonewa.

Pia amelitaka jeshi la polisi kuacha kutumika kukandamiza haki za raia kwani wajibu wake ni kulinda mali na haki zao.

Amesema tangu kuingia kwa serikali ya awamu ya tano matukio mbalimbali ya kusikitisha  yameongezeka kinyume na utamaduni mzuri ambao nchi ilikuwa ikiujenga.

“Matukio ya watu kupotea katika mazingira ya kutatanisha, kutekwa na kuteswahasa na jeshi la polisi sasa yamekuwa sehemu ya maisha ya watanzania, hali hii haikubaliki na tumeona tujitokeze na kuchukua wajibu wa kusema na kukemea ili kulinusuru taifa na hatari inayolinyemelea,” amesema.

Akizungumzia kuhusu mfumo wa vyama vingi, ameitaka serikali kutenda haki kwa vyama vya siasa kufanya kazi zao kwa uhuru  ni takwa la kikatiba na si hisani ya watawala.

Pamoja na mambo mengine ngome hiyo imetoa mapendekezo sita, kurejesha mchakato wa katiba mpya kwani ndiyo itakuwa jibu la msingi kwa changamoto zinazolikabili taifa.

Mengine, imeitaka serikali kuacha kujenga mazingira kandamizi na hofu, kutishia wananchi (wanyonge), kuwanyanyasa kiasi kwamba wanashindwa kupumua na kufaidi utanzania uliojengwa katika misingi ya utu na heshima kwa binadamu wote bila kujali vyama, dini na ukabila.

Pia imetaka kuundwa kwa tume huru ya uchaguzi ili kusaidia kufanya uchaguzi huru na wa haki.

About Author Matukio360

Matukio360 ni sehemu pekee inayokuletea matukio ya moto moto kutoka pande zote za dunia katika wakati ule ule yalipotokea yaani mubashara. Habari ni za uhakika na zilizofanyiwa uchunguzi wa kina na kuandikwa kwa ueledi mkubwa na sio ukanjanja. Usibanduke katika ukurasa huu wa Matukio360, wajulishe na marafiki zako sasa wajipatie habari za uhakika.

No comments:

Post a Comment

Leo leo Plus

Start typing and press Enter to search